SEHEMU ya Shule ya Mivumoni Islamic Seminary iliyoko ndani ya Msikiti wa Mtambani, Kinondoni jijini Dar es Salaam, imeteketea kwa moto, asubuhi ya leo Jumamosi tarehe 18 Julai 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kwa mujibu wa Mariki Balongo, Mwalimu wa shule hiyo, moto huo ulianza majira ya saa 9:30 asubuhi, katika stoo ya shule hiyo.
Mwalimu huyo amesema, hakuna mwanafunzi aliyeathirika na tukio hilo, bali baadhi ya vifaa vya shule na vya wanafunzi viliteketea kwa moto.
Hata hivyo, Balongo amesema chanzo cha moto huo bado hakijajulikana.
“Ni kweli moto ulitokea sehemu ya stoo ya shule, ulianza saa tatu na nusu asubuhi. Hakuna mwanafunzi aliyedhurika lakini baadhi ya vifaa viliungua,” amesema Balongo.
Amesema moto huo ulidhibitiwa na kikosi cha zimamoto na uokoaji, kilichofika shuleni hapo saa 10:30 asubuhi.
“Chanzo cha moto hakijulikani nini hadi sasa. Na sidhani kama itakua umeme sababu kwenye hiyo stoo hakuna swichi zaidi ya taa ambayo swichi yake iko nje,” amesema Balongo.
Leave a comment