KAMATI ya maadili ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imewapiga faini kiasi cha Shilingi 5 milioni, Msemaji wa klabu ya Simba, Haji Manara na mjumbe wa bodi ya wakurugenzi wa klabu hiyo, Zacharia Hanspope kuhusu sakata la kesi ya mchezaji, Bernard Morrison. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Akisoma hukumu hiyo mbele ya waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Wakili, Mwita Waisaka amesema kuwa licha ya kupigwa faini ya fedha hizo lakini wawili hao wamepewa onyo kali na kutotakiwa kutenda kosa la kimaadili katika kipindi cha miaka miwili.
Manara aliitwa mbele ya kamati hiyo mara baada ya kuongea maneno ya kutuhumu, kutishia na kuingilia majukumu ya kamati hiyo kupitia kipindi kituo cha radio cha Wasafi FM kwenye kipindi cha Sports Arena kinachoruka kila siku kuanzania jumatatu mpaka Ijumaa.
“Mnamo tarehe 11 agosti, 2020 Manara alilalamikiwa na kutuhumu, kutishia na kuingilia majukumu ya kamati ya sheria na haki za wachezaji kinyume na kanuni ya 73 ya maadili, kitendo hicho kilipelekea kuchafua taswira ya kamati na kuishushia hadhi TFF.
“Kamati ilifikia maamuzi ya kumtoza fani ya shilingi 5 milioni Haji Manara na kumpa onyo kali kwa kutotenda kosa la kimaadili katika kipindi cha miaka miwili,” alisema Wakili huyo.
Kwa upande wa hukumu ya Hanspope, Wakili Waisaka alisema kuwa kiongozi huyo alisomea shtaka la kutoa taarifa ya shauli huku likiendelea kusikilizwa akijua ni kinyume na utaratibu kupitia kipindi cha michezo cha Wasafi FM.

“Akiwa mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo alisikika kwenye vyombo vya habari akitoa taarifa ya shauri hilo ambalo lilikuwa likisikilizwa huku akijua kuwa hana mamlaka hayo isipokuwa hidhini ya Mwenyekiti kitendo kilichopelekea kuchafua taswira ya kamati na hadhi za wachezaji,” alisema Wakili Waisaka.
Adhabu hiyo zimekuja kufuatia sakata la mchezaji, Bernad Morrison alipokuwa na mgogoro wa kimkataba na klabu yake ya zamani ya Yanga na mchezaji huyo kushinda kesi hiyo na kuzinishwa kuwa mchezahi halali ya klabu ya Simba.
Leave a comment