JOHN Mongela, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, amewataka maofisa elimu wa shule za msingi na sekondri mkoani humo, kuwapeleka wanafunzi kushiriki na kujifunza utamaduni wa nchi katika tamasha la Urithi Festival. Anaripoti Charles Mseti, Mwanza … (endelea).
Tamasha hilo lenye kauli mbiu ya ‘Urithi Wetu Fahali Yetu,’ linatarajiwa kufanyika kitaifa kuanzia tarehe 31 Oktoba hadi 2 Novemba 2019 katika viwanja vya Rock City Mall jijini humo.
Mongella ametoa kauli hiyo leo tarehe 29 Oktoba 2019, alipozungumza na wanahabari kuhusu kilele cha tamasa hilo na kuwa, tamasha hilo lenye lengo la kutambua na kutangaza sanaa na utamaduni wa nchi (Tanzania), litazidi kurudisha uzalendo kwa wananchi.
“Wananchi wote wa mikoa jirani ya Mwanza, wote nina wakaribisha kuja kutambua sanaa na utamaduni wa nchi yetu pamoja na kutangaza sanaa za nchi yetu.
“Niwatake maofisa elimu wa shule zetu za msingi na sekondari, waje na wanafunzi wao katika hili tamasha, kuja kuona utamaduni wetu na sanaa yetu, hii itasaidia kurudisha uzalendo kwa watoto wetu,” amesema Mongella.
Amesema katika tamasha hilo pia kutakuwa na michezo mingine ya mashindano ya baiskeli na mchezo wa bao. hata hivyo Novemba 3 mwaka huu kutakuwa na safari ya kutembelea hifadhi ya Taifa ya Burigi iliyopo Chato mkoani Geita.
Tamasha hilo limeshirikisha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Wizara ya Maliasili na Utalii na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza. Mgeni rasmi katika kilele cha tamasha hilo anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Leave a comment