NASEEB Abdul ‘Diamond Platnumz’ atakiwa kufika mahakamani Oktoba 30, 2017 kujibu malalamiko ya kushindwa kumuomba radhi mzazi mwenzake, Hamisa Mobetto na kushindwa kutoa matunzo ya mtoto, anaandika Mwandishi Wetu.
Diamond amepelekwa wito wa kuitwa mahakamani na mawakili wa Mabetto, Abdullah Zulu na Walter Godluck kutoka Kampuni ya Uwakili ya Century Attorneys.
Katika wito huo Diamond Platnumz anadaiwa kumdhalilisha na kutompa matumizi ya mtoto kwa takribani miezi miwili.
Zulu amesema mteja wao Hamisa Mobetto alimtumia Diamond notisi ya kumuomba radhi na kumtaka apeleke matunzo ya mtoto ndani ya siku saba.
“Baada ya kuona kimya tulipeleka kesi katika Mahakama ya Kisutu upande wa watoto (The Juvenile Court Of Dar es Salaam) na leo (Alhamisi) tumepewa barua ya wito na tayari mwanasheria wa mwanamuziki huyo ameipokea,” amesema.
Kesi hiyo itaanza kusikilizwa Oktoba 30, mwaka huu.
Leave a comment