MWENYEKITI wa Klabu ya Simba, Mohamed Dewji ‘MO Dewji’ amesema, mchezaji wao, Clatous Chama ataendelea kuhudumu klabuni hapo hadi mwaka 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
MO Dewji amesema hayo leo Jumapili tarehe 15 Novemba 2020 wakati anazungumza na waandishi wa habari akitoa mrejesho wa kikao cha bodi ya ligi kilichofanyika jana Jumamosi.
Amesema, kumekuwa na maneno mengi yanayoendelea mitandaoni kuhusu kiungo huyo raia wa Zambia, Chama kujiunga na watani zao, Yanga hali inayoipua presha kwa mashabiki na viongozi wa mabingwa hao watetezi wa ligi kuu ya vodacom Tanzania Bara.
“Kumekuwa na kelele nyingi sana kuhusu Chama mara (Meddie) Kagere, sisi Simba tumejipanga na hili la Chama amekwenda sijui Yanga, Chama tumesaini nae mtakana mpaka 2022. Hii hoja ya Chama imeishia hapa,” amesema MO Dewji.
Amesema “Kuna propaganda zinaendelea. Kuna gazeti nimesoma Chama amevaa jezi ya Yanga, ujue tusiende na mambo ya barabarani, sisi Simba hatuwezi kuropoka ropoka hovyo, sisi mambo ya Chama tumekwisha maliza.”
Katika kusisitiza hilo, amesema “Chama tumemalizana naye mapema, hatukutaka kutangaza, lakini hizi propaganda zisizo na maana hazifai.”
Leave a comment