RAIS wa heshima na mwekezaji wa klabu ya Simba Mohammed Dewji “MO” amefunguka kuwa klabu hiyo tayari imeshaanza mazungumzo na baadhi ya wachezaji wakiwemo Victorien Adebayor na Moses Phiri kwa ajili ya kujiunga na kikosi cha mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu kwa msimu ujao. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mo ameyasema hayo hii leo tarehe 11 Machi 2022, wakati akiongea na mashabiki wa klabu hiyo kwa njia ya mtandao kuelekea mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya RS Berkane ya nchini Morocco.
Mchezo huo ambao utapigwa siku ya jumapili, tarehe 13 Februari 2022, kwenye dimba la Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, ambapo mgeni rasmi atakuwa Omar Said Shaaban, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda wa Zanzibar.
Akijibu swali juu ya usajili wa wachezaji hao, mwekezaji huyo alifunguka kuwa kwa upande wa Adebayor anaonekana kuwa mchezaji mzuri na tayari kamati ya usajili imeshaanza kuongea nae na anaweza kucheza Simba kwa msimu ujao.
“Ni mchezaji mzuri lakini yeye mwenyewe ana hamu ya kuja kucheza Simba, kwa hiyo kamati ya usajili wameshaanza kuongea nae na kama makubaliano yatafikiwa anaweza kucheza Simba msimu ujao.” Alisema MO
Mchezaji huyo ambaye alionesha kiwango kizuri kwenye mchezo wa kwanza, ulipigwa nchini Nigeria ambapo Simba ilishuka dimbani dhidi ya USGN na kwenda sare ya bao 1-1.
Kwa upande wa Moses Phiri anayekipiga kwenye klabu ya Zanaco ya nchini Zambia, mwekezaji huyo alisema kuwa mchezaji huyo bado wanamfuatilia na kama mambo yatakaa sawa atajiunga na mabingwa hao.
“Mambo ya usajili lazima yafanywe kwa akili kubwa na siri kubwa. Kwenye miaka hii minne tumejifunza mengi sana, naomba mtuamini kwamba hao wachezaji tunawafatilia kwa karibu kwahiyo muda ukifika tutawambia.” Alisema Bilionea huyo
Phiri alianza kufuatiliwa na klabu za Simba na Yanga, toka kwenye dirisha dogo la usajili mara baada ya kuonesha kiwango bora alipotua nchini kwenye mchezo wa wiki ya Mwananchi dhidi ya Yanga, lakini ilkuwa ngumu kuondoka Zanaco kwa kuwa bado walikuwa wanashiriki michuano ya kimataifa na mkataba wake ulisalia mwaka mmoja.
Leave a comment