CHANZO cha ugomvi uliosababisha kifo cha Esther Gadeu anayedaiwa kuuawa na mumewe, Godbles Sawe kimetajwa kuwa ni madai ya wivu wa kimapenzi uliotokana na mke kudai talaka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Sawe anadaiwa kumwua mkewe tarehe 14 Juni 2022 saa 12 jioni nje ya nyumba yao.
Akizungumza na MwanaHALISI Online nyumbani kwake Mwananyamala, Dar es Salaam, mama wa marehemu Esther, Consolva, alisema binti yake alikuwa akidai talaka kwa mumewe, kwa muda mrefu.
Alisema ugomvi huo uliwafikisha mahakamani, “pale mahakamani mwanangu alishindwa.”
Esther ni mtoto wa pili wa familia ya watoto wanne wa Consolva na Benito Gadeu.
Akifafanua kuhusu mkasa huo, Consolva alisema, “mwanangu alidai mahakamani kuwa pamoja na kuachwa, basi aishi na watoto wake na Mahakama ikampa ushindi mumewe Sawe wa kubaki na nyumba na watoto.”
Alisema kitendo hicho kilimfanya mwanawe huyo akate rufaa na kuendelea kulea watoto wake hapo hapo nyumbani wakati akisubiri uamuzi wa rufaa yake na watoto wake wakue.
Mama Esther aliendelea kusimulia kuwa kilichosababisha umauti wa mwanawe, ni kuendelea kukaa kwenye nyumba ya Sawe ambapo jioni ya tarehe 14 Juni 2022, Sawe alifika na kung’oa mihogo iliyopandwa na Esther.
“Esther alimhoji sababu ya kuharibu mazao waliyopanda, Sawe akamshambulia na kusababisha kifo chake,” alisema mama huyo.
Tukio hilo lilithibitishwa kutokea na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro na kueleza kuwa mtuhumiwa wa mauaji hayo bado anatafutwa.
Akisimulia tukio hilo, Diwani wa Kibamba, Peter Kilango alisema kuwa mtuhumiwa alifanya tukio hilo saa 12.30 jioni akitumia jembe kumkata kichwani na kukimbilia kusikojulikana, akitumia usafiri wa bodaboda.
Diwani Kilango alisema mtuhumiwa huyo anajishughulisha na ufundi wa friji na siku ya tukio mtuhumiwa alitoka nyumbani na kumwacha mkewe, akikanda unga wa ngano kwa ajili ya kuchoma maandazi.
“Mke wake ni mjasiriamali anafanya kazi ya kuchoma maandazi na vitumbua, na wakati anatengeneza vitu vyake kwa ajili ya kuchoma maandazi na vitumbua, alitoka na kwenda kununua mkaa,” alisema Kilango.
Aliongeza, kuwa baada ya Esther kurudi, alikuta mlango umefungwa na kushangaa kuwa nani amefunga, mwanamke huyo aliuliza majirani na kujibiwa kuwa mumewe alipogundua ni wake, alikwenda kwa mjumbe, kwa kuwa hawakuwa na uhusiano mzuri na mumewe.
Alieleza, baada ya mjumbe kuelezwa, alikuja na kugonga mlango na mtuhimwa akafungua na kumwamuru mkewe aingie ndani, lakini mkewe akakataa kuingia. Aliongeza, kwamba kwa kuwa majirani wanafahamu ugomvi wao, waliondoka wakiamini kuwa wataelewana.
“Wakati wakiwa nje ya nyumba yao mtuhumiwa akamwita mtoto wao, Ben anayesoma darasa la saba Kibamba, lakini mkewe akamjibu hayupo amemtuma dukani.
“Jibu hilo lilimkasirisha mumewe wakati ameshikilia jembe akijifanya analima, na ghafla akamkimbiza mkewe na kumpiga nalo kichwani,” aliongeza Kilango.
Baada ya kuanguka, mtuhumiwa alimponda kichwa mithili ya mtu anayelima, hali iliyosababisha fuvu kupasuka.
Wananchi waliposhituka na kujaribu kumkamata, alikimbia na kufika barabarani na kupanda bodaboda na kutokomea kusikojulikana.
MwanaHALISI Online ilifika Kibamba shuleni ambako Esther alikuwa akiishi na ndipo alikofia, lakini ilikuta nyumba imefungwa ukimya ukiwa umetawala.
Mwandishi wa habari hii alifika nyumbani kwa Chanzo Sabinus ambaye ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Kibamba Shule ambaye pia ni mjumbe wa eneo hilo.
Sabinus alilimbia gazeti hili kuwa nyumba hiyo imefungwa na hakuna jirani atakayetoa ushirikiano kwa chombo chochote cha habari.
Jirani mwingine aliyeomba kutotajwa jina, alikieleza chombo hiki kuwa Sawe hakuwa na ushirikiano wala uhusiano mzuri na jirani zake tofauti na mkewe Ester.
“Yaani sijui nisemeje, wengejua hao ndugu wa Esther, sisi tulikuwa tunaishi naye kama ndugu yetu,” Sabinus alisema.
Leave a comment