MKUU wa Jeshi la Magereza nchini Kamishna Jenerali Mzee Ramadhani Nyamka amewataka wahitimu wa kidato cha nne wa Shule ya Sekondari Bwawani iliyopo mkoa wa Pwani kuwa na tahadhali dhidi ya mimba za utotoni na maambukizi ya ugonjwa hatari wa ukimwi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Kamishna Nyamka aliyasema hayo mwishoni mwa wiki kwenye mahafali ya 19 ya kidato cha nne katika shule hiyo inayolilikiwa na Jeshi la Magereza ambapo aliwataka wahitimu kuepukana na vishavishi vya aina yoyote kwani vina athari kubwa kwa jamii.
“Ugonjwa wa ukimwi na mimba za utotoni vimekuwa ni tishio kwa taifa, waathirika wengi ni vijana hasa watoto wa kike ambao ndiyo nguvu kazi ya kujenga taifa,”alisema Nyamka.
Alisema ni wazi kuwa hata malengo waliyojiwekea katika maisha yao yatakuwa hayana maana iwapo wahitimu hao wataruhusu ukimwi uwaondoe duniani na wao kukosa elimu, hivyo amewataka kuepukana na vishawishi na makundi yasiyofaa.
Nyamka alisema ukimwi hauna tiba hivyo aliwataka wahitimu na wanafunzi wanaendelea kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya janga hilo na kwamba njia iliyobora ni kuepukana na tamaa.
Aidha, Mkuu huyo wa Magereza aliupongeza uongozi wa shule hiyo kutokana na taaluma nzuri iliyopo shuleni hapo ambapo alisema atahakikisha kuwa shule hiyo inakuwa miongoni mwa shule zinazofanya vizuri mitihani ya taifa kila mwaka.
Kamishna Nyamka alitoa vyeti kwa wahitimu 126 na kutaka wawe mabalozi wa shule hiyo kwa kutangaza mazuri yote waliyoyapata shuleni hapo ili jamii yote kwa ujumla inufaike na uwepo wa Shule ya Bwawani.
Naye Mkuu wa Shule hiyo, ACP Anthony Sogoseye alisema taaluma ya shule hiyo imekuwa ikipanda kila mwaka na kwamba siri kubwa ya mafanikio hayo ni kujituma kwa walimu kufundisha, nidhamu kwa wanafunzi pamoja na ushirikiano kwa uongozi wa shule na wazazi.
Aidha, Mkuu huyo aliwataka wazazi kuhakikisha wanalipa ada mapema, ili kuepuka kumrudisha mwanafunzi nyumbani kufuata ada kwani kitendo hicho kunarudisha nyuma maendeleo ya kitaalima.
Nao wazazi wenye watoto shuleni hapo akiwemo Sarah Robert aliwashukuru walimu wa shule hiyo kwani mbali na taaluma wanaoitoa kwa wanafunzi wao pia wamesaidia kujenga nidhamu kwa watoto na kuwa vijana wa mfano kwa jamii.
Leave a comment