JESHI la Polisi Wilayani Tarime mkoa wa Mara, wamewahoji viongozi watano wa chama cha Chadema wilayani humo, kwa tuhuma za kutoa lugha za uchochezi katika mkutano wa Mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko uliofanyika jana tarehe 7 Aprili 2019. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Viongozi hao wa Chadema akiwemo Katibu wa Chadema mkoani Mara, Mwalimu Chacha Heche na Katibu wa chama hicho jimbo la Tarime, Peter Magwi wamehojiwa leo tarehe 8 Aprili 2019 katika Kituo Kikuu cha Polisi wilayani Tarime cha Bomani.
Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE, Magwi amesema wamehojiwa kituoni hapo kwa tuhuma za kutoa lugha za uchochezi na kuzidisha muda wa kufanya mkutano.
Magwi amesema wamekwisha maliza kuhojiwa na kwamba wanafuatalia taratibu za kupatiwa dhamana.
“Tumehojiwa kituo cha Bomani kuhusu mkutano wa jana wa Matiko, tuhuma tulizohojiwa ni kutoa lugha za uchochezi na kuzidisha muda wa mkutano,” amesema Magwi.
Mtandao huu ulimtafuta Kamanda wa Polisi Mkoani Mara, Henry Mwaibambe kwa ajili ya kupata taarifa zaidi za mahojiano ya viongozi hao wa Chadema kwa njia ya simu, lakini iliita pasipo kupokelewa.
Kwa taarifa zaidi kuhusu dhamana za viongozi hao, usikose kufuatilia mtandao huu.
Leave a comment