MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Sengerema mkoani Mwanza, Magesa Mafuru amewataka watendaji katika ofisi ya Ofisa maendeleo ya jamii kujitathimini katika utendaji wao wa kazi kutokana na kutuhumiwa kutoa mikopo kwa vikundi kwa upendeleo kinyume na utaratibu. Anaripoti Moses Mseti … (endelea).
Mkurugenzi huyo ametoa kauli hiyo leo wakati akitoa hundi ya mikopo yenye thamani ya Sh. 42 milioni kwa vikundi 30 vya akinamama wilayani humo, fedha ambazo zinatokana na mapato ya ndani.
Amesema Halmashauri ya Sengerema ina kata 26 vijiji 71 vitongoji 419 na kila sehemu kuna akinamama ambao nao wanatakiwa kunufaika na mikopo inayotolewa na serikali ili wajikwamue kimaisha.
Amesema anashangazwa kuona kila mwaka vikundi vinavyopewa mikopo ni vile vile huku akidai watu walipewa dhamana hiyo ya kusimamia utoaji mikopo wakitoa kinyume na utaratibu.
Mafuru amesema utendaji kazi wa mratibu wa mfuko wa wanawake unatia mashaka hivyo anatakiwa kubadilika na kutoa fursa sawa kwa wanawake wote wilayani humo na kumtaka kujitathimi utendaji kazi wake.
”Siwezi kutoa mkopo tena, endapo hakutakuwa na vikundi vya akinamama wengine kutoka kata zingine, kila mikopo inatolewa hapa mjini tu inanitia mashaka tunapaswa kubadirika,” amesema Mafuru.
Mwenyekiti wa wanawake wajasiliamali, Halmashauri ya Sengerema, Daline Matonange amekiri kuwepo kwa madhaifu hayo huku akiwataka watendaji kubadilika juu ya suala hilo na kufuata maelekezo waliyopewa na mkurugenzi huyo.
Mratibu wa Mfuko wa Wanawake wajasliamali wilayani humo, Noela Yamo alipotakiwa kujibu tuhuma hizo, amesema yeye ni sehemu ya watumishi wa halmashauri hiyo anayetakiwa kuzungumzia swala hilo ni afisa maendeleo ya jamii na siyo yeye licha ya baadhi ya vikundi kumtupia lawama kuwa anatoa mikopo kwa upendeleo.
Kaimu Ofisa Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya Sengerema, Boniphace Kasasilo amesema maelekezo yote waliyopewa watayazingatia na kuyafanyia kazi na kuondoa dosari zilizojitokeza na kuvitaka vikundi vinavyodaiwa kurejesha mikopo kwa haraka.
Leave a comment