KIUNGO wa Simba, Jonas Mkude na nyota wa Yanga, Bernard Morrison wamefungiwa kucheza michezo miwili pamoja na faini ya Sh. 500,000 kwa makosa ya utovu wa nidhamu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Maamuzi hayo yametoka chini ya Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), chini ya Mwenyekiti wake, Peter Hella ambaye alisoma maamuzi hayo.
Mkude amefungiwa mara baada ya kumpiga kiwiko mchezaji wa timu ya Biashara ya Mara, kwenye mchezo wa Ligi Kuu iliyochezwa tarehe 22 Februari, 2020 kwenye Uwanja wa Taifa.
Morrison aliingia kwenye adhabu hiyo baada ya kumpiga kiwiko mchezaji wa Tanzania Prisons kutoka Mbeya na adhabu hizo zitaanza mara moja.
Klabu hizo zitaanza kuwakosa wachezaji hao kwenye michezo ya leo ya Ligi Kuu, ambapo Simba itashuka dimbani kuikabili Mbeya City, huku Yanga watakuwa Uwanja wa Taifa, kuikaribisha Namungo FC kutoka Lindi.
Leave a comment