MKAZI wa kata ya Magamba wilayani Songwe mkoani Songwe, Kabula Kuba ambaye pia ni mjane, ameibuka katika Mkutano wa Mkuu wa mkoa huo, Omary Mgumba na kudai Kituo kipya cha afya Magamba kimejengwa katika eneo la ardhi ambayo ni mali ya mumewe. Anaripoti Mwandishi Wetu, Songwe … (endelea).
Akizungumza katika mkutano huo ambao ni moja ya mikutano ya ziara ya Mkuu huyo wa Mkoa, Kuba amesema eneo la ardhi hiyo palipojengwa kituo hicho limeporwa kwa mumewe bila taarifa.
“Mkuu wa Mkoa mimi ni mjane, nina watoto sita…mmoja ni mlemavu. Hiki Kituo kimejengwa kwenye aneo tulilolimiki mimi na mume wangu ambaye alishafariki. Kimejengwa tena hata bila kunishirikisha, nakuomba unisaidie mjane mimi nipate haki yangu,” alisema Kabula.
Awali kabla ya kutoa uamuzi Mgumba alimkaribisha Diwani wa kata ya Magamba, Kapala Makelele ili atolee ufafanuzi ambapo kwa upande wake diwani huyo alishindwa kutoa maelezo yaliyokamilika hali iliyosababisha wananchi kumzonga kwa kelele na kumtaka aeleze ukweli.
Kutokana na hali hiyo Mkuu huyo wa Mkoa alilazimika kuwauliza wananchi juu ya eneo hilo mmiliki ni nani ambapo kwa pamoja wananchi hao walikiri eneo hilo ni la mjane Kabula.
Aidha, kutokana na majibu hayo, Mgumba aliwaagiza viongozi wa Magamba kukaa chini na mjane huyo ili kuangalia jinsi ya kulimaliza tatizo hilo.
Alisema kituo hicho kimegharimu fedha nyingi zaidi ya milioni 500 hivyo hawezi kubomoa bali busara itumike ili kumaliza mgogoro huo.
Leave a comment