TANZANIA imepokea msaada wa dawa pamoja na vifaa tiba vyenye thamani ya Sh.864 milioni vitavyosaidia kupambana dhidi ya magonjwa mbalimbali kutoka katika Serikali ya Misri. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Ndege iliyobeba shehena ya vifaa hivyo, imetua leo Ijumaa tarehe 14 Januari 2022, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
Balozi Misri nchini Tanzania, Mohamed Gaber Abouelwafa amekabidhi shehena hiyo kwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Profesa Abel Makubi kwa niaba ya Waziri wa wizara hiyo, Ummy Mwalimu.
Akipokea msaada huo, Prof. Makubi amesema, msaada huo umeletwa baada ya ziara ya kikazi ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kutembelea nchini Misri Novemba 2021.
“Tunamshukuru sana Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Tanzania pamoja na Serikali ya Misri kwa kushirikiana na Tanzania hasa katika kuboresha sekta ya afya kwa kusaidia mahitaji mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa dawa na vifaa tiba,” amesema Profesa Makubi.
Aidha, Profesa Makubi amesema msaada huo utaenda kuwasaidia wananchi wenye uhitaji katika vituo mbali mbali vya kutolea huduma za afya nchini.
Kwa upande wake, Balozi wa Misri nchini Tanzania, Mohamed Gaber Abouelwafa amesema kujitoa kwa Serikali ya Misri, kusaidia sekta ya afya ni kutokana na jitihada za Rais Samia katika kuwaletea maendeleo wananchi, ikiwemo kuboresha sekta ya afya nchini kwa kupambana dhidi ya magonjwa.
“Serikali ya Misri itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kusaidia maendeleo ya Watanzania, hasa katika kuboresha sekta ya afya, hii inatokana na nia njema ya Mhe. Rais Samia katika kuleta maendeleo kwa wananchi, hususan katika kuboresha Sekta ya afya,” amesema Balozi Abouelwafa.
Amesema, uongozi makini chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, Serikali ya Misri imetoa ahadi kuendelea kusaidi Sekta ya Afya nchini kwa kuendelea kuleta Dawa pamoja na vifaa tiba kwaajili ya kupambana dhidi ya Magonjwa mbalimbali.
Leave a comment