LICHA ya fedha za miradi ya maendeleo katika sekta ya ujenzi kutolewa kwa asilimia 96.48, utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa barabara na madaraja nchini Tanzania umekuwa wa kusuasua. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hadi Aprili, 2022 fedha zilizopokelewa ni Sh. 1.532 sawa na asilimia 96.48 ya fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha 2021/22
Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2022/23, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Makame Mbarawa, amesema Wizara kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ilipanga kujenga barabara kuu zenye urefu wa kilometa 467.11 kwa kiwango cha lami, lakini hadi Aprili 2022 ni kilometa 216.26 zimekamilika sawa na asilimia 46.
Pia amesema Wizara ilipanga kujenga madaraja 14 pamoja na ukarabati wa kilometa 32.47 kwa kiwango cha lami katika barabara kuu lakini hadi Aprili 2022 imefanya ukarabati wa kilometa 2.5 sawa na asilimia 8 za Barabara Kuu.
Ameongeza utekelezaji wa miradi ya madaraja ya Kiyegeya (Morogoro), Daraja Jipya la Selander mkoani Dar es Salaam, Kitengule mkoani Kagera na Ruhuhu mkoani Ruvuma mekamilika na madaraja mengine yapo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Kwa upande wa barabara za mikoa, amesema Wizara kupitia TANROADS ilipanga kujenga kwa kiwango cha lami jumla ya kilometa 103.0 ambapo kilometa 72.2 zilipangwa kujengwa kwa kutumia fedha za Mfuko Mkuu wa Serikali na kilometa 30.8 zilipangwa kujengwa kwa fedha za Mfuko wa Barabara.
Amesema kazi nyingine ni ukarabati kwa kiwango cha changarawe jumla ya kilometa 1,124.3.
Hata hivyo hadi Aprili, 2022 ni kilometa 34.8 za barabara za mikoa zilijengwa kwa kiwango cha lami na jumla ya kilometa 307.41 zilikarabatiwa kwa kiwango cha changarawe.
Mbarawa amesema utekelezaji wa miradi uliathiriwa kwa kuchelewa kupatikana kwa misamaha ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Leave a comment