KIUNGO mshambuliaji wa Simba, Luis Miquissone pamoja na mlinzi wa kati, Pascal Wawa wamerejea kikosini baada ya kukosa mchezo uliopita wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Gwambina FC. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Wachezaji hao wanarejea uwanjani kesho kwenye mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Dodoma Jiji utakaopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa saa 1 kamili usiku.
Akiongea mbele ya waandishi wa habari leo kuelekea mchezo huo wa kesho kocha msaidizi wa Simba, Seleman Matola amesema kuwa wachezaji hao watakuwa sehemu ya kikosi kwenye mchezo wa kesho mara baada ya kukaa nje kwa kutumikia adhabu ya kadi tatu za njano.
“Kwenye mchezo wa kesho tutamkosa Thadeo Lwanga ambaye alipata msiba wa dada yake, ila Pascal Wawa pamoja na Luis Miquissone wamerejea kikosini mara baada ya kumaliza adhabu zao za kadi tatu za njano,” alisema Matola.
Aidha kuelekea mchezo huo wa kesho kocha huyo, alisema kuwa wamejipanga vizuri na kuhakikisha kupata ushindi ili waendelee kutetea taji lao la Ligi Kuu Tanzania Bara ambao wao ni mabingwa watetezi.
Kwa upande wa nahodha msaidizi wa timu hiyo, Mohamed Hussein ameeleza kuwa wao kama wachezaji wamejipanga kuondoka na alama tatu kwenye mchezo wa kesho dhidi ya Dodoma Jiji.
“Tupo uwanja wa nyumbani na tutautumia vizuri na makocha wameshatupa maelekezo yao jinsi gani tunavyotakiwa tucheze ili kesho tupate pointi tatu muhimu,” alisema nahodha huyo.
Simba inaingia kwenye mchezo wa kesho huku ikiwa kileleni kwenye msimamo wa Ligi hiyo wakiwa na pointi 58, huku nafasi ya pili ikishikwa na Yanga wenye pointi 57 na nafasi ya tatu wapo Azam FC wakiwa na pointi 54.
Leave a comment