Milipuko miwili imetokea katikati mwa jiji la Kampala nchini Uganda na kujeruhi watu kadhaa ambao idadi yao haijajulikana. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea)
Mlipuko huo umetokea leo asubuhi tarehe 16 Novemba, 2021 na kusababisha mtikisiko mkubwa kwenye jumba la maduka karibu na kituo cha Polisi cha Central wakati mwingine umetokea karibu na Bunge la nchi hiyo.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la BBC, majengo ya ofisi yalitikisika wakati milipuko hiyo ilipoanza.
Aidha, Gazeti la nchini humo, Daily Monitor limesambaza video ya magari yakiungua nje ya jengo la bima baada ya mlipuko huo.
Wakati Televisheni ya NTV ya nchini humo ambayo inarusha matangazo ya moja kwa moja kwenye barabara ya bunge ikisema spika na maafisa wengine walikuwa wamehamishwa na polisi waliokuwa wamezingira eneo hilo.
Chanzo cha milipuko hiyo na majeruhi, bado haijathibitishwa.
Mwezi uliopita, milipuko miwili tofauti nchini humo iliua watu wawili. Mmoja ulimuua mhudumu katika baa na mwingine, mshambuliaji wa kujitoa mhanga ambaye alikuwa ameingiza vilipuzi kwenye basi.
Mamlaka nchini humo zimeshutumu milipuko hiyo ya Oktoba dhidi ya kundi la waasi wa Kiislamu lenye makao yake makuu nchini Uganda, DR Congo, Allied Democratic Forces.
Takriban watu 50 wamekamatwa, na wengine kushtakiwa mahakamani, tangu matukio hayo ya hivi majuzi.
Leave a comment