ZAINABU Mohamed Jabir, mtumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), amekamatwa kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa ya Sh.50 milioni. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa iliyotolewa na Doreen Kapwani, Msemaji wa Takukuru, leo Ijumaa, tarehe 30 Aprili 2021, imesema, Zainabu aliomba rushwa kutoka kwa mtu mmoja ili kumsaidia katika tuhuma dhidi yake, zinazochunguzwa na taasisi hiyo.
“Uchunguzi dhidi ya tuhuma hii unaendelea na utakapokamilika hatua stahiki zitachukuliwa,” amesema Doreen.
Taarifa hiyo ya Doreen, aliyoitoa kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali John Mbungo imetoa onyo kwa watu ambao wamekuwa wakijitambulisha kama watumishi wa taasisi hiyo.
Amesema, matapeli hao, wamekuwa wakiwapigia watu simu na kujitambulisha kwamba ni watumishi wa Takukuru kwamba wanapaswa kufika ofisini kuhojiwa, wakati si kweli.
Amewataka wananchi, wanapopokea simu za aina hiyo, kufika ofisi za Takukuru kujua ukweli zaidi.
Leave a comment