TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) nchini Tanzania, imemkamata ofisa wake wa uchunguzi mwandamizi, Nina Sipilon Saibul kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa ya Sh.4.9 milioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kinondoni … (endelea).
Taarifa iliyotolewa jana Ijumaa tarehe 11 Septemba 2020 na Doreen Kapwani, Ofisa Uhusiano wa Takukuru imesema, Nina alikamatwa jana Alhamisi.
Doreen alisema, Nina ambaye ni Afisa Uchunguzi ofisi ya Takukuru Kinondoni jijini Dar es Salaam, aliomba rushwa kutoka kwa mfanyabiashara mmoja wa Jiji hilo anayejishughulisha na shughuli za Real Estate.
“Takukuru Mkoa wa Kinondoni, ilipokea taarifa za malalamiko dhidi ya afisa wake, kuomba rushwa ili asiendelee na uchunguzi uliodaiwa ulikuwa ukiendelea ndani ya Takukuru dhidi ya mfanyabiashara huyo(mlalamikaji).”
“Baada ya taarifa hizo kupokelewa, uchunguzi wa awali wa kuthibitisha tuhuma hizo ulifanyika na kubaini upo ukweli wa madai ya kuomba hongo lakini hakukuwa na jalada wala uchunguzi wowote uliokuwa ukiendelea dhidi ya mlalamikaji,” amesema Doreen.
Alisema, Takukuru imechukua hatua hii ili kuhakikisha inajisafisha dhidi ya watumishi wake wachache wenye tabia ovu zenye kukichafua chombo hicho.
“Uchunguzi dhidi ya tuhuma hii unakamilishwa ili kuweza kuwafikisha watuhumiwa mahakamani mapema iwezekanavyo,” alisema Doreen.
Leave a comment