MIKOA yote nchini imeagizwa kutenga maeneo kwaajili ya kilimo kikubwa cha mazao ambayo yanayostawi katika mikoa hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Maagizo hayo yametolewa leo tarehe 8 Agosti, 2022 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, katika kilele cha maadhimisho ya sikukuu ya wakulima maarufu Nane Nane yaliyofanyika mkoani Mbeya kitaifa.
Amesema Wizara imejipanga kupitia miradi ya umwagiliaji maji na kupitia kilimo cha mashamba makubwa kuingiza vijana katika kilimo ili kupunguza utegemezi kutoka nje wa mazao ya mafuta, ngano na sukari.
“Nilipokuwa pale Kagera nikizindua eneo moja la kiwanda cha sukari nilitoa wito kwa mikoa kutenga maeneo ya kilimo tunahitaji hekta zaidi ya 150,000 kwaajili ya kilimo kikubwa cha mablock kwaajili ya mazao ya kimkakati ya Chikichi, alizeti, soya na ngano,” amesema Rais Samia.
Amesema tayari wameanza mkoa wa Dodoma na wanafuatia Mbeya, “nitake mikoa yote ipange eneo kubwa kwa lile zao ambalo litamea vizuri na kuzalisha kwa tija.”
“Niombe sana ule uzalishaji wa vipande vipande tuende navyo lakini tujielekeze kwenye kilimo cha biashara kilimo kikubwa,” amesema.
Leave a comment