SERIKALI imeombwa kutoa elimu kwa viongozi wa ngazi za vijiji ili waweze kusimamia na kuzitumia sheria ndogo za ardhi zilizopo kwa ajili ya migogoro ya ardhi, anaandika Christina Haule.
Ombi hilo lilitolewa jana na wakulima wa kata ya Hembeti wilayani Mvomero mkoani Morogoro wakati wa mdahalo wa siku tatu wa elimu shirikishi kwa umma juu ya utatuzi wa migogoro ya ardhi.
Viongozi mbalimbali wakiwemo wenyeviti wa vijiji, kata na vitongoji, katika kata za Hembeti, Mvomero na Dakawa wilayani Mvomero walishiriki.
Akizungumza wakati akichangia mada ya umuhimu wa sheria za ardhi, Yusufu Mabela amesema suala la migogoro ya ardhi katika vijiji vya kata ya Hembeti bado ni janga linalohitaji msaada mkubwa kutatuliwa.
“Kwa sasa watu wa Hembeti wanaonekana wadhaifu zaidi sababu hawawezi kusogelea mashamba yao licha ya kutengewa kwa sababu wafugaji wameyamiliki yote na mkulima ukionekana huko ni kipigo” amesema Mabela.
Naye Diwani wa kata ya Hembeti Peter Mdidi amesema hakuna kijiji ambacho hakina sheria za ardhi na kwamba zilizopo zinashindwa kutekelezeka.
Leave a comment