SERIKALI ya Awamu ya Tano tangu ilipoingia madarakani tarehe 5 Novemba 2015, imeteua, kutengua ama kuwabadili makamishna wakuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Katika kipindi cha miaka takribani mitano ya Serikali ya Awamu ya Tano, iliyoongozwa na Hayati John Magufuli na sasa Samia Suluhu Hassan, TRA imeongozwa na makamishna wakuu sita.
Hayati Magufuli aliingia madarakani tarehe 5 Novemba 2015, akipokea kijiti kutoka kwa Jakaya Kikwete. Amekuwa Rais hadi tarehe 17 Machi 2021 alipotangazwa kufariki dunia katika Hospitali ya Mzena, mkoani Dar es Salaam.
Akiwa madarakani, Hayati Magufuli aliteua, tengua ama kuhamisha mabosi wanne wa TRA, lengo likiwa kuimarisha taasisi hiyo nyeti yenye jukumu la kukusanya kodi.
Alipoingia madarakani, TRA ilikuwa ikiongozwa na Rished Bade, lakini ilipofika tarehe 27 Novemba 2015, alimsimamisha kazi na kumteua Dk. Philip Mpango kukaimu nafasi hiyo.
Hayati Magufuli, alichukua uamuzi huo kufuatia ziara aliyoifanya Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa bandarini na kubaini upotevu wa makontena 349.

Hayati Magufuli alimtaka Bade kutoa ushirikiano kwa Dk. Mpango wakati uchunguzi ukiendelea.
Dk. Mpango alikaimu nafasi hiyo hadi tarehe 24 Desemba 2015, alipomteua kuwa mbunge na Waziri wa Fedha na Mipango.
Nafasi hiyo ya Dk. Mpango ambaye sasa ni Makamu wa Rais wa Tanzania, aliteuliwa Alphayo Kidata kuwa Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA.

Kidata ambaye baadaye alithibitishwa kuwa kamishna mkuu, alihudumu nafasi hiyo hadi tarehe 23 Machi 2017, alipoteuliwa kuwa Katibu Mkuu Ikulu.
Nafasi hiyo, ilikaa wazi kwa takribani siku nne hadi tarehe 27 Machi 2017, alipoteuliwa Charles Kichere, ambaye awali, alikuwa naibu kamishna mkuu.
Kichere alihudumu nafasi ya Kamishna Mkuu wa TRA hadi tarehe 8 Juni 2019, alipotenguliwa na Hayati Magufuli kisha akamteua kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Njombe.

Nafasi ya Kichere ambaye kwa sasa ni Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), aliteuliwa Dk. Edwin Mhede.
Kabla ya uteuzi huo wa Dk. Mhede, alikuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara.
Mara baada ya kifo cha Rais Magufuli, Samia aliyekuwa Makamu wa Rais, aliapishwa tarehe 19 Machi 2021, kuwa Rais wa Tanzania kumalizia muda uliobaki wa Serikali ya Awamu ya Tano.

Rais Samia ambaye anaendelea kupanga safu ya uongozi kwa viongozi mbalimbali, ameigusa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ambapo Jumapili ya tarehe 4 Aprili 2021, alimteua Alphayo Kidata, kurejea kuiongoza TRA.
Hii ina maana mpaka sasa, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya marais, Hayati Magufuli na Samia, TRA imeongozwa na makamisha sita ambao ni Rished Bade, Dk. Philip Mpango, Alphayo Kidata, Charles Kichere, Dk. Edwin Mhede na Alphayo Kidata.
Leave a comment