CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimemtaka Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi, atimize ahadi yake ya kuondoa siasa za uhasama visiwani humo, kwa kuwa wananchi wanahitaji maendeleo na si chuki zinazowagawa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Wito huo umetolewa jana Jumatano na Katibu wa Habari, Uenezi, Mawasiliano na Umma wa ACT-Wazalendo, Salum Bimani, akituma salamu za chama hicho kuelekea maadhimisho ya miaka 59 ya Mapinduzi ya Zanzibar, yanayayoadhimishwa leo tarehe 12 Januari 2023.
“Chama kinapenda kumkumbusha Rais Mwinyi kauli yake aliyotoa wakati akifungua Baraza la Wawakilishi kwamba wananchi wetu wamechoshwa na siasa za uhasama, kuhubiri chuki na visasi ambazo hazibadilishi hali ya maisha yao kuwa bora zaidi. Wanataka matunda ya mapinduzi na si simulizi za mapinduzi na muungano,” imesema taarifa ya Bimani.
Taarifa ya Bimani imesema kuwa, ACT-Wazalendo kinaamini kwamba Zanzibar haiwezi kufikia maendeleo bila ya kuwepo azma njema ya kulinda heshima, uhuru, haki, usawa, umoja na mshikamano pamoja na utawala wa sheria na maridhiano.
Aidha, chama hicho kimetoa mapendekezo 10 kwa Serikali ya Rais Mwinyi , ikiitaka iyafanyie kazi haraka kwa ajili ya kuimarisha maridhiano na Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).
Miongoni mwa mapendekezo hayo ni, kufanya mapitio ya sera, sheria na taratibu zinazochangia kuongeza ugumu wa hali ya maisha ya wananchi ikiwemo kodi na tozo, uvunja mizizi ya unyanyasaji na uvunjaji wa haki za binadamu.
Mengine ni, kuondoa ufisadi na urasimu katika taasisi za umma, kuunda upya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Ili kuifanya iwe huru na kuunda upya Sheria ya Uchaguzi Zanzibar, Ili izingatie matakwa ya demokrasia ya vyama vingi.
“ACT-Wazalendo inaitaka Serikali kuzifanyia marekebisho Idara maalum za umma ili zisitumike kisiasa na kufanya marekebisho makubwa katika mfumo wa utumishi wa umma ili kuwe na ufanisi katika kutoa huduma kwa wananchi,” imesema taarifa ya Bimani.
Leave a comment