POLISI wilayani Mazabuka mkoa wa Kusini nchini Zambia wamemtia mbaroni mhudumu wa chumba cha kuhifadhia maiti (mochwari) katika Hospitali Kuu ya Mazabuka kwa tuhuma za kudaiwa kuchezea maiti hiyo na kuchuna ngozi ya mkono mmoja. Anaripoti Mwanishi Wetu … (endelea).
Hata hivyo, mhudumu huyo baada ya kubanwa aliijitetea kuwa panya ndio wameitafuna ngozi ya mkono wa maiti hiyo jambo ambalo limepingwa na ndugu wa marehemu ambao pia wamegoma kuzika mwili wa ndugu yako.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Naibu Kamishna wa Polisi wa Mkoa wa Kusini, Alfred Nawa amesema mhudumu huyo alichukuliwa kutoka hospitalini jana tarehe 18 Septemba na kusafirishwa kwenda kuhojiwa lakini pia kulinda usalama wake.
Amesema uchunguzi wa awali baada ya mtaalamu wa magonjwa kuuchunguza mwili huo, amesema hakuna alama za mnyama yeyote kutafuna ngozi ya mkono huo.
Nawa ambaye amelihifadhi jina la mhudumu huyo amesema pamoja na hayo, mtuhumiwa ataachiwa huru baada ya mahojiano.
Mwili huo wa marehemu aliyefahamika kwa jina la Benson Mooya, 62, mkazi wa Mazabuka aliyefariki tarehe 15 Septemba aliyetarajiwa kuzikwa tarehe 17 Septemba, 2021 lakini ndugu wa marehemu waligoma kuendelea na mazishi wakitaka uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo.
Ndugu hao wamedai majibu ya uongozi wa hospitali hiyo hayakuwaridhisha hivyo wameapa kutozika mwili wa ndugu yao hadi daktari atakapochunguza zaidi kwani hawaamini kama panya amehusika.
Diwani wa Kata Mazabuka, Crispin Hamangaba naye ameiomba Serikali kuingilia kati na kurejesha ubora wa huduma katika taasisi ya afya nchini humo.
Leave a comment