WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama amesema Serikali haitosita kumchukulia hatua za kinidhamu na kisheria kiongozi yeyote atakayeshindwa kusimamia vizuri rasilimaliwatu kwa ajili ya ustawi wa Taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Mhagama amesema hayo leo tarehe 20 Disemba, 2022 wakati wa kikao kazi chake na watumishi wa umma katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro.
Kikao hicho kililenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi katika halmashauri hiyo.
Amesema, hatomuonea aibu wala huruma kiongozi yeyote aliyepewa dhamana ya kusimamia rasilimaliwatu ambaye atabainika kukiuka sheria na taratibu za usimamizi wa rasilimaliwatu.
Ameongeza kuwa, viongozi wenye dhamana ya kusimamia rasilimaliwatu wanapaswa kuiheshimu, kuithamini na kuhakikisha inakuwa kwenye mikono salama kwasababu inategemewa na Serikali kwa kiasi kikubwa katika ustawi na maendeleo ya taifa.
“Rasilimaliwatu ambayo ndio watumishi wa umma ikisimamiwa vizuri itaisaidia Serikali kutimiza lengo la kutoa huduma bora kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kutekeleza mipango na mikakati ya maendeleo katika taifa,” amefafanua.
Amesisitiza kuwa watumishi wa umma ndio wanategemewa kutoa huduma bora za afya, kuboresha huduma za maji, kuboresha huduma za elimu, kuboresha huduma za miundombinu pamoja na kilimo.
Akizungumza kwa niaba ya watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Mwenyekiti wa Chama cha Walimu Kilosa, Mwalimu Richard Shagungu ameishukuru Serikali kwa kuendelea kulipa kila mwezi madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi katika Halmashauri hiyo na kuomba waajiri wasizalishe madai mapya ili Serikali iyamalize madai yaliyopo sasa.
Mhagama amefanya ziara ya kikazi ya siku moja katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa ili kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa umma na kukagua utekelezaji wa mpango wa TASAF.
Leave a comment