JENISTA Mhagama, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Sera, Ajira, Vijana na Wenye ulemavu amemwagiza Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na waajiri nchini, kumwandalia ripoti ya taasisi za umma pamoja na mashirika ambayo bado hayajaunda Mabaraza ya Wafanyakazi. Anaripoti Danson Kaijage, Dar es Salaam … (endelea).
Mhagama alitoa maagizo hayo tarehe 14 Januari 2021, jijini Dodoma wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu Taifa cha Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (TALGWU).
Alisema, taasisi nyingi za umma bado hazijaunda mabaraza ya wafanyakazi, hali ambayo inanyima wafanyakazi haki yao ya msingi kujadiliana mambo yanayohusu haki zao.
“Msajili nataka uniandalie ripoti haraka sana, maeneo mengi bado hayana mabaraza ya wafanyakazi. Maeneo kama Osha pamoja na Tarura bado hawana mabaraza haya, kwanini hawana mpaka sasa? inabidi niipate ripoti hiyo haraka,” alisema Mhagama.
Aidha, alisema mabaraza yana umuhimu mkubwa kwa wafanyakazi kwa kuwa ni eneo ambalo linawapa fursa ya kujadili haki zao na kero mbalimbali ambazo wanazipata kutoka kwa waajiri wao.
Pia aliwataka wafanyakazi wote kuungana na serikali katika kupinga matumizi mabaya ya fedha za umma.
“TALGWU mnafanya vizuri sana katika kudhibiti matumizi mabaya ya fedha zenu, lakini hili mnatakiwa kulifundisha kwa wafanyakazi wetu kule wanakofanya kazi kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria na kanuni,” alisema.
Vile vile, Mhagama alisema wafanyakazi wa serikali za mitaa ndiyo wamekuwa wakikutana na wananchi wa hali ya chini katika utendaji wao wa kila siku, hivyo wanaowajibu wa kuwa waadilifu katika maeneo yao.
“Kila siku wananchi wanakuta na maofisa watendaji wa vijiji, wauguzi, maafisa mifugo, maafisa kilomo hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa kuzingatia miiko ya utumishi wa umma na kutenda haki kwa watanzania wanyonge,” alieleza Mhagama.
Mkuu wa kitengo cha mawasiliano kimataifa wa TALGWU, Shan Kibwasali akisoma risala kwa niaba ya Katibu Mkuu Taifa, alisema kuwa moja ya matatizo wanayokumbana nayo ni watumishi wastaafu kutolipwa fedha za kurejea nyumbani mara baada ya kustaafu, pia kucheleweshewa mafao yao.
“Suala hili limekuwa ni kero hasa baada ya kuunganishwa kwa mifuko ya hifadhi ya jamii, hivyo tunakuomba waziri utusaidie kuziangaza mamlaka husika kutatua suala hili ili watumishi walipwe mara baada tuu ya kustaafu kwa mujibu wa sheria,” alieleza Kibwasali.
Leave a comment