JACOB Paul Nyangusi, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) nchini Tanzania, itamfunguliwa kesi ya Uhujumu Uchumi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), baada ya kukutwa na tuhuma za rushwa ya ngono. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Leo Alhamisi tarehe 13 Agosti 2020, Takukuru Mkoani Dodoma inamfikisha mhadhiri huo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, kujibu mashtaka yanayomkabili ya Uhujumu Uchumi kwa kosa la kutaka rushwa ya ngono.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo imetolewa leo na Sosthenes Kibwengo, Mkuu wa Takukuru mkoani Dodoma, Nyangusi amekwenda kinyume na kifungu cha 25 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11/2007.
“Takukuru kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, tutamfikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodom a Nyangusi (43) na kumfungulia shauri la Uhujumu Uchumi kwa kosa la kutaka rushwa ya ngono kinyume cha sheria,” inaeleza taarifa ya Kibwengo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kibwengo, Takukuru ilimkamata Nyangusi usiku wa tarehe 3 Oktoba 2018 nyumbani kwake maeneo ya nyumba 300 jijini Dodoma, muda mfupi kabla ya kutekeleza nia yake ovu ya kufanya ngono na aliyekuwa mwanafunzi wake wa mwaka wa kwanza.
Tukio hilo lilitekelezwa na Takukuru baada ya taasisi hiyo kupokea taarifa kwamba mhadhiri huyo alimtaka mwanafunzi wake kingono kama sharti la kumsaidia ili aweze kufanya mitihani ya marudio na kumwezesha kufaulu katika somo lake.
“Na ndipo Takukuru ikaweka mtego na kumkamata. Baada ya uchunguzi kukamilika Ofisi ya Tiafa ya Mashtaka kuridhia kwa mujibu wa sheria ndipo mtuhumiwa anafikishwa mahakamani,” inaeleza taarifa ya Kibwengo.
Leave a comment