MGOMBEA urais katika Uchaguzi mkuu wa Kenya na wakili msomi Profesa George Wajackoyah ameendelea kujinadi kwa ahadi zenye utata kwa Wakenya baada ya kuahidi kukuza soko la biashara kati ya nchi hiyo na China kwa kuwauzia Wachina nyama ya fisi hususani korodani. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mgombea huyo ambaye alijizolea umaarufu kwa kuahidi kuhalalisha bangi nchini humo, pia kuanzisha biashara ya nyama ya nyoka na mbwa, jana tarehe 30 Juni, 2022 amesema raia wa china hutumia korodani za fisi kama dawa.
Akizindua ilani yake ya Uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Agosti mwaka huu, ameahidi kwamba akiwa rais atahakikisha ameimarisha uhusiano wa kibiashara na Uchina.
“Tutauza nyama ya fisi kwa Uchina, kwa sababu sisi hatuhitaji fisi katika Kenya hii. Mchina anakula fisi,” alisema Wajackoyah.
Msomi huyo aliendelea kudadavua zaidi suala hilo ambapo alitoa takwimu kwamba Kenya kuna fisi zaidi ya 1000 na kila fisi ana korodani mbili, hivyo Kenya itavuna fedha za kutosha a kigeni.
“Mimi nasikia fisi 1000 wa kiume, wako na korodani 2000. Na mimi nasikia hizo korodani ni dawa kwa China. Hizo korodani ni za gharama kubwa zaidi kushinda hata Ganja (bangi). Korodani moja ni karibu milioni sita (TSh milioni 119). Kwa hiyo tutauza China korodani za fisi, nyama ya mbwa na nyama ya nyoka,” amesema Prof. Wajackoyah huku umati uliokuwa umefurika kwenye ukumbi wa KICC ukimshangilia kwa kelele zisizojua kikomo.
Prof. Wajackoyah pia alizidi kudadavua zaidi kwamba gharama ya bei ya mbwa iko juu zaidi kuliko hata nyama ya mbuzi na ng’ombe ambazo taifa la Kenya linauza nje ya nchi.
“Kilo moja ya nyama ya mbwa inauza mara sita zaidi ya bei ya nyama ya mbuzi kilo moja. Kenya inauza nje nyama ya mbuzi na ng’ombe kule Mashariki ya kati. Kwa hiyo acha nisisitize hapo tena, nyama ya nyoka inaenda Uchina, wakishakula, deni tumelipa,” alisisitiza Wajackoyah.
Leave a comment