WAKILI Victoria Mandari, ambaye ni miongoni mwa wagombea wa Urais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) amesema anaamini wagombea wa nafasi hiyo ambao ni wanasiasa hawataingiza maslahi ya vyama vyao iwapo watashinda, anaandika Charles William.
Akizungumza mapema leo asubuhi katika kipindi cha Power Breakfast cha Clouds FM, Victoria amesema TLS inaendeshwa kwa kanuni na taratibu zake na hivyo kumekuwepo wa hofu kuwa wagombea ambao ni wanasiasa wanaweza kuivuruga TLS.
“Watu wamekuwa na hofu, ya kwamba iwapo wanasiasa wataiongoza TLS basi watashindwa kutenganisha maslahi ya vyama vyao lakini nadhani TLS ni taasisi imara yenye kanuni zake na kila kiongozi atatakiwa kuzifuata,” amesema.
Victoria ameeleza kuwa uchaguzi wa TLS mwaka huu umekuwa na hamasa kubwa zaidi kutokana na uwepo wa wagombea ambao ni wanasiasa, waliowahi kuwa watumishi serikalini pamoja na mawakili wakongwe.
“Chama chetu kipo tangu mwaka 1954 na kimekuwa kikifanya chaguzi tangu miaka hiyo, lakini mwaka huu kumekuwa na hamasa na msisimko zaidi,” amesema.
Victoria amesisitiza kuwa ingawa yeye ni mgombea pekee mwanamke kati ya wagombea watano na pia hajulikani ni mwanachama wa chama gani cha siasa lakini hatatumia mambo hayo kama vigezo vya kuombea kura.
“Sihitaji kura za huruma, mawakili wanawake ni wengi lakini sitaomba kura za wanawake, kwasababu sigombei kwenda kutetea maslahi ya wanawake bali maslahi ya mawakili wote hapa nchini,” amesema.
Wagombea watano waliopitishwa na kamati ya uchaguzi ya TLS ni Tundu Lissu ambaye ni Mbunge na Kiongozi wa kambi ya Upinzani Bungeni, Lawrance Masha ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani katika serikali ya awamu ya nne, Godwin Mwapongo ambaye ni kada wa Chama Cha Mapinduzi, Francis Stolla ambaye ni Rais wa TLS anayegombea kutetea kiti chake na Mwanamama Victoria Mandari.
Uchaguzi wa TLS unatarajia kufanyika Jumamosi ya tarehe 18 Machi mwaka huu, katika Ukumbi wa AICC, Arusha ambapo mawakili wote hapa nchini watapata nafasi ya kupiga kura ya kuchagua viongozi wao.
Leave a comment