AISHA Madoga, mgombea ubunge katika Jimbo la Dodoma mjini kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ameahidi kuboresha sekta ya elimu, afya na maji. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Madoga ametoa ahadi hiyo tarehe 20 Septemba 2020, jijini humo wakati chama hicho kikizindua kampeni za ubenge Dodoma mjini, katika kata ya Chang’ombe.
Amesema, akichaguliwa kuwa mbunge wa jimbo hilo atahakikisha elimu inapewa kipaumbele ili kuwezesha watoto kupata elimu bora na sio bora elimu.
Amesema, hivi sasa elimu nchini inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa madawati, vyumba vya madarasa, nyumba za walimu, uhaba wa walimu hasa katika masomo ya Sayansi pia matundu ya vyoo.
“Mimi nikiwa mbunge wa jimbo hili, nitahakikisha kuwa hizo changomto zote tunazifanyia kazi ili watoto wetu waweze kusoma katika mazingira mazuri na yatakayowawezesha kujifunza katika mazingira rafiki kuliko sasa ,”amesema.
Pia, Madoga ameeleza kuwa kero, nyingine atakayoifanyia kazi ni sekta ya maji ambapo atahakikisha, anaikomesha kwa kuboresha miundombinu ya huduma za maji ikiwa ni pamoja na uchimbaji wa visima hasa katika maeneo ya vijijini.
“Hivi sasa maji imekuwa ni changamoto kubwa sana hasa katika maeneo ya vijijini, mimi nikiwa mbunge nitahakikisha kwa kushirikiana na wadau wengine huduma za maji zinaboreshwa ili kuwasaidia akamama ambao wamekuwa wakitembea umbali mrefu kila siku”amesema Madoga.
Vile vile amesema, kutokana na elimu kuwa ufunguo wa maisha, yeye kama mwakilishi wa wananchi, atahakikisha kuwa maeneo yote yenye changamoto anayafanyia kazi katika kipindi chake cha ubunge na kubaki historia.
Aidha, amesema katika sekta ya afya atahakikisha kuwa wananchi wanapata huduma za matibabu yaliyo bora katika maeneo wanayoishi, na kundoa adha ya kutembea umbali mrefu kufuata matibabu.
“Sekta ya afya ndiyo msingi wa maendeleo, mtu bila kuwa na afya bora hawezi kushiriki hata katika shughuli za maendeleo. Hivyo, mimi nitahakikisha kuwa suala la sekta ya afya linakuwa kipaumbele change,”amesema. Madoga
Chama hicho kimezindua rasmi kampeni zake za unbunge katika jijini Dodoma, baada ya mgombea wake wa ubunge kurejeshwa na Tume ya Taifa ya uchaguzi (NEC) baada ya rufaa yake kukubaliwa.
Tanzania hii ni nchi ambayo Mungu ametupa sote na tunahitaji kuheshimiana kwa mkubwa na mdogo pia ili tuijenge nchi yetu ikiwa na amani, upendo, umoja, utulivu na usawa kwa kila mmoja wetu. Viongozi wetu na wagombea mnaohitaji kuiongoza nchi hii na watu wake kumbukeni yupo Mungu mwenye nguvu juu yako ambaye hafurahishwi na midomo yenu inayotoa matusi na kejeli kwa upande mwingine kwa wanaotaka madaraka au walio kwenye madaraka. Mimi najua yupo mwenye nchi hii ambaye ni Mwenyezi Mungu pekee, sisi ni wapiga debe wa maisha fulani tu. Wito wangu kwenu waungwana fanya mambo ambayo hata mbele za Mungu wa mbingu na nchi yanaleta utukufu.