UPANDE wa wajibu maombi katika kesi Na. 570/2023, iliyofunguliwa na wajumbe wa zamani wa Bodi ya Wadhamini ya Chama cha NCCR- Mageuzi, umeweka mapingamizi ya awali dhidi yake, ukiitaka Mahakama Kuu, Masjala Kuu ya Dar es Salaam, kuitupilia mbali kwa madai kuwa imefunguliwa kinyume cha sheria. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mapingamizi hayo yamewekwa leo Jumanne, tarehe 24 January 2023, na Wakili wa wajibu maombi, Novatus Mhangwa wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kusikikizwa mahakamani hapo mbele ya Jaji Ephery Kisanya.
Kesi hiyo ilifunguliwa na wajumbe wa zamani wa bodi hiyo wanaodaiwa kufukuzwa NCCR-Mageuzi, dhidi ya wajumbe wanaodaiwa kuwa wapya, wakipinga uteuzi wao kwa madai kuwa ulikuwa kinyume cha sheria , ambapo wanaiomba mahakama itamke wajumbe wapi halali.
Katika pingamizi la kwanza, Wakili Mhangwa anadai kwamba kesi hiyo imefunguliwa kinyume cha sheria Kwa kuwa waleta maombi wamefungua bila kutoa taarifa ya kusudio la kuishtaki Serikali, ndani ya siku 90.
Amedai kuwa, Sheria ya Mashauri ya Serikali iliyofanyiwa marejeo 2019, inaelekeza mtu anayekusudia kuishtaki Serikali, atoe taarifa ya kusudio kwa njia ya maandishi siku 90 kabla ya shauri kufunguliwa mahakakani.
Katika pingamizi la pili, Wakili Mhangwa amedai waleta maombi walikiuka Sheria kufungua kesi hiyo kwa kumshtaki Msajili wa Vyama vya Siasa nchini.
Akikazia hoja hiyo, mwakilishi wa mjibu maombi wa sita, Faustine Sungura, ameiomba mahakama iitupilie mbali kesi hiyo kwa madai kwamba waleta maombi wamemlalamikia Msajili wa Vyama vya Siasa, badala ya kumuunganisha katika kesi ili apate nafasi ya kusikilizwa.
Amedai kuwa, katiba ya nchi kinakataza mahakama kumwadhibu mtu ambaye hajapewa haki ya kusikilizwa.
Sungura ametaja pingamizi la tatu kuwa ni, waleta maombi wamekimbilia kufungua kesi mahakamani badala ya kufuata hatua za kukata rufaa ndani ya chama chao.
Amedai kuwa, waleta maombi walipaswa kukata rufaa dhidi ya uteuzi wa wajumbe wapya wa bodi hiyo, katika Mkutano Mkuu wa NCCR-Mageuzi, uliofanyika tarehe 24 Septemba 2022.
Pingamizi la mwisho lililowasilishwa na Sungura, lilidai kwamba waleta maombi wamekosea kutamka jina la Mwansheria Mkuu wa Serikali katika hati yao ya kiapo, kwa kuwa wamemtaja kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali, badala ya kumtaja kama Mwansheria Mkuu wa Serikali.
Hata hivyo, mawakili wa Serikali, waliomba mahakama iyatupilie mbali mapingizi hayo kwa madai kwamba hayakuwa na msingi, Ili kesi ianze kusikilizwa.
Kwa upande wake mleta maombi namba moja, Mohamed Tibanyendera ameiomba mahakama hiyo iyatupilie mbali mapingamizi hayo kwa madai kwamba yanalengo kuzuia haki kutendeka.
Kuhusu pingamizi lililodai waleta maombi walitakiwa kutoa taarifa ya kusudio la kuishtaki serikali siku 90 kabla ya kufungua kesi mahakamani, Tibanyendera ameiomba mahakama ilitupe.
Kwa madai kwamba sharti Hilo hutumika pale ambapo mtu anamalalamiko dhidi ya Serikali na kwamba wao hawana malalamiko hayo, Bali wanaiomba mahakama itamke nani mjumbe halali wa Bodi ya Wadhamini ya NCCR-Mageuzi.
Katika kesi hiyo, waleta maombi wanaishtaki Serikali kupitia Wakala wa Usajili wa Vizazi na Vifo (RITA) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Wajumbe hao wa zamani wakiwemo Mohamed Tibanyendera, Thomas Nguma, Samuel Ruhuza na Mose Juma Faki, walifukuzwa uanachama pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, Francis Mbatia.
Ambapo wamefungua kesi hiyo dhidi Beati Mpitabakama na anayedaiwa kuwa Kaimu Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, Joseph Selasini. Wengine ni, Laila Rajab na Idrissa Omary.
Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa, endelea kufuatilia MwanaHALISI Online
Leave a comment