MBUNGE wa Viti Maalum, Catherine Magige (CCM) amehoji kuhusina na ni lini serikali itatatua mgogoro wa Pori Tengefu la Loliondo uliodumu zaidi ya miaka 25, anaandika Dany Tibason.
Akiuliza swali leo bungeni, Catherine alidai kuwa katika Pori Tengefu wa Loliondo kumekuwa na mgogoro mkubwa hivyo ni lini serikali itatatua mgogoro huo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Ramo Makani amesema Desemba 2016, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alifanya ziara katika Wilaya ya Ngorongoro ambapo pamoja na mambo mengine alitoa maelekezo ya jinsi ya kupata ufumbuzi wa mgogoro huo.
Amesema katika utelekezaji wa agizo hilo kamati maalum shirikishi inayoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha ambapo iliundwa ili kupata mapendekezo ya namna ya kutatua migogoro hiyo.
‘’Kamati maalum ilifanya kazi yake kwa njia mbalimbali zikiwemo kufanya vikao na wadau mbalimbali kutembelea eneo lenyewe ili kujua hali halisi na kuandaa taarifa yenye mapendekezo ya namna kutatua mgogoro huo,’’ amesema
Naibu Waziri huyo amesema mapendekezo ya kamati hiyo yamewasilishwa kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Leave a comment