KAMATI ya Uongozi ya chama cha ACT-Wazalendo imeonesha kutofurahishwa na namna ya teuzi za John Magufuli, Rais wa Tanzania zinavyofanyika bila mashauriano na wahusika katika vyama, Jambo hilo limepekea Kamati hiyo kumtaka Rais kuweka mfumo bora wa kuazima watu kutoka vyama vingine, anaandika Hamisi Mguta.
Samson Mwigamba, Kaimu Kiongozi wa chama hicho leo ameyasema hayo wakati akitoa maamuzi ya kikao cha Kamati hiyo juu ya uenyekiti ndani ya chama ikiwa ni siku chache baada ya rais kumteua na kumuapisha Anna Mghwira, Mwenyekiti wa chama hicho kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro bila ya kufanya mashauriano na viongozi wa chama.
“Ili kusimamia maendeleo ya nchi ni vyema kufanya mashauriano na vyama husika ili kuepusha migongano isiyo ya lazima ndani ya vyama na jamii,”amesema Mwigamba.
Aidha, amesema kuwa kutokana na mashauriano ndani ya chama, Mghwira amekoma kuwa Mwenyekiti wa chama na kumteua Yeremia Maganja kuwa Kaimu Mwenyekiti wa chama hadi uchaguzi utakapoitishwa mwezi Machi 2018 hivyo Mghwira atabaki kuwa mwanachama huku akiendelea kutumikia nafasi mpya ya Mkuu wa Mkoa.

Mwigamba amesema, uteuzi huo wa pili kufanywa na Rais Magufuli katika chama hicho baada ya mwanzoni kumteua Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji ni kielelezo kuwa chama kina watu makini na wanaofaa kuongoza.
Tazama Video hapo chini mwanzo mwisho …
Julius Mtatiro, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi CUF aliwahi kusema kuwa uteuzi wa wa Mghwira haukupaswa kufanywa bila mashauriano kwakuwa viongozi wa chama kimoja kuteuliwa kujiunga na serikali ya chama kingine hufanywa kwa heshima kubwa.
“Kwa kawaida, Rais alipaswa kuwasiliana na Kiongozi Mkuu wa chama na kumjulisha nia hiyo, hata kama Kiongozi Mkuu wa ACT na chama chake wangelikataa, Rais angelikuwa ametimiza wajibu wake wa Ustaarabu wa Kidemokrasia.
“Ndiyo maana, Katibu Mkuu wa UN alipotaka kumteua Dk. Rose Migiro kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UN kwanza aliomba ruhusa kwa Rais Kikwete (Rais aw Tanzania), huo ndiyo utaratibu ikiwa uteuzi unafanywa kwa nia njema,” alisema Mtatiro.
Leave a comment