HUSNA Sekiboko, mbunge wa viti maalum, aiomba Serikali ya Tanzania, kufanya marekebisho ya mtaala wa elimu ya msingi na sekondari. Anaripoti Jemima Samwel DMC … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa, leo Ijumaa, tarehe 4 Juni 2021, katika kipindi cha maswali na majibu bungeni jijini Dodoma.
Sekiboko amesema, Serikali inapaswa kutambua umuhimu wa kufanya marekebisho ya mtaala ya ngazi hiyo ili kuendana na uhitaji wa sasa.
“Je, ni lini Serikali itafanya marekebisho ya malengo ya mtaala wa elimu ya Msingi na Sekondari nchini ili kuendana na uhitaji wa sasa?”
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Juma Kipanga amesema, Serikali inatambua umuhimu wa kufanyia marekebisho Mitaala ya Elimu ya Msingi na Sekondari ili kuwawezesha wanafunzi kupata stadi mbalimbali zinazoendana na mahitaji ya wakati.
“Kwa sababu hiyo, Serikali imekuwa ikiboresha mitaala hiyo kila kunapokuwa na hitaji la kisayansi, kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kiteknolojia.”
“Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imepanga kufanya mjadala mpana kuhusumfumo wa Elimu nchini ambao utahusisha Sera ya elimu na mitaala kwa ujumla ili iendane na wakati na ikidhi mahitaji ya sasa na baadae,” amesema Kipanga.
Kipanga amesema, katika mjadala huo mpata “tutakwenda kuudadavua na kuuweka kwenye mawanda mapana” ili malengo ambayo wadau mbalimbali wa elimu wanataka, yanakwenda kufanyiwa kazi.
Leave a comment