MEYA wa Manispaa ya Kinondoni (CCM), Songoro Mnyonge pamoja na Mkurugenzi wa manispaa hiyo, Sipora Liana, wamemaliza mgogoro wao uliobuka hivi karibuni, kuhusu makusanyo ya fedha za ushuru wa takataka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Leo Ijumaa tarehe 21 Mei 2021, Viongozi hao wamepatanishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla, siku moja baada ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo, kuagiza Kamati za Siasa na uongozi wa chama hicho mkoa, kuwashughulikia viongozi na watendaji wa manispaa walioko katika migogoro.
Taarifa ya Kitengo cha Habari cha Mkoa wa Dar es Salaam, imesema wawili hao waliitwa na Makalla, kwa ajili ya kujadili chanzo cha mgogoro wao, ulioibuka juzi tarehe 19 Mei 2021, katika Kikao cha Baraza la Madiwani la Manispaa ya Kinondoni.
“Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam, amemaliza sintofahamu ya uongozi wa manispaa ilijitokeza kati ya Mnyonge na Sipora. Utatuzi wa mgogoro huo umefanyika leo katika kikao cha pamoja kilichoitishwa na mkuu wa mkoa na kuwakutanisha meya na mkurugenzi,” imesema taarifa hiyo.
Katika kikao hicho, Makalla aliwataka viongozi hao kurejea katika majukumu yao ya usimamizi wa utekelezaji Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/2025.
“Mkuu wa mkoa amewataka viongozi hao kurejea ofisini na kufanya kazi kwa pamoja, kutekeleza miradi ya maendeleo na kutatua kero za wananchi,” imesema taarifa hiyo.
Kwa upande wa Songoro na Sipora, wamemaliza tofauti zao na wameahidi kufanya kazi kwa pamoja kwa maslahi mapana ya wananchi na nchi.
Mvutano huo uliibuka baada ya Sipora, kutuhumu kuwa katika manispaa hiyo kuna genge la wezi, akidai kuna mtandao wa wizi wa fedha za ushuru wa takataka.
Kufuatia tuhuma hizo, Songoro alimtaka atoe ushahidi katika kikao hicho, juu ya tuhuma hizo ili vyombo vya ulinzi na usalama vichukue hatua.
Baada ya kauli hiyo, Sipora alisema ana uthibitisho kuhusu sakata hilo, akidai kuwa alifanya uchunguzi uliobainisha namna baadhi ya watendaji wa manispaa hiyo, wanavyofanya ubadhirifu katika ukusanyaji wa ushuru wa takatakata.
Mkurugenzi huyo wa Kinondoni alidai, watendaji hao wasiokuwa waaminifu huwapa risiti wananchi zenye viwnago vidiogo ikilinganishwa na fedha wanazotozwa.
“Wale watu walikuwa wamepewa kazi ya kukusanya mapato ya takataka, wakawa wanatoza wananchi 2,000, 1,000 na 3,000 lakini risiti wanazotoa zimeandikwa 100, 200 na 300. Wananchi wakaandamana kuja ofisini kwangu wakaleta risiti,” alisema Sipora.
Sipora alisema “nikatuma watu wangu kuchunguza wakabaini ni kweli wananachi wamelipa 1,000, 2,000 na 3,000. Tukaja kwenye mfumo wa kaprinti kuanzia mwaka jana Julai, tukaona katika kila risiti wamechukua 900, 1,800 na 2700.”
Leave a comment