MEYA wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita leo amezuiwa kuhudhuria kikao cha Kamati ya Mipango Miji, Mazingira na Usafirishaji kilichopangwa kufanyika kwenye ukumbi wa Karimjee. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Meya Isaya alifika kwenye ukumbi huo leo tarehe 23 Januari 2020, ili kuhudhuria kikao hicho, alizuiwa na askari wa jiji kuingia ukumbuni, kwa madai hatambuliwi.
Taarifa zaidi zinaeleza, licha ya Halmashauri ya Jiji kuitisha kikao hicho, Meya Isaya hakualikwa ingawa ni mjumbe wa kamati hiyo.
Meya Isaya alipofika lango la ukumbi, alizuiwa na askari wa jiji na kumtaka aondoke. Kutokana na zuio hilo, purukushani ziliibuka na kusababisha askari mmoja kutishia kupiga risasi.
Askari huyo hakusema atampiga risasi nani, lakini alikoki silaha yake kisha akasema “nampiga mtu risasi.”
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya tukio hilo, Meya Isaya amedai, walinzi waliomzuia walitumwa na mkurugenzi wa jiji Sipora Liana.
Mkaka mwandishi anaondoka eneo la tukio, Meya Isaya na mwenyekiti wa kikao hicho Patrick Asenga na baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo, walikuwa nje ya ukumbi.
Tarehe 9 Januari 2020, kilifanyika kikao kilichokuwa na agenda ya kujadili tuhuma zilizokuwa zinamkabili Meya Isaya, ikiwemo za matumizi mabaya ya ofisi, kwa ajili ya kumchukulia hatua.
Lakini kikao hicho kiliibua vurugu, baada ya wajumbe wa upande wa upinzani kupinga mchakato uliotumika kuendesha kikao hicho, kilichotangaza kumvua madaraka Meya Isaya.
Wajumbe hao walipinga kikao hicho kwa maelezo kwamba, hakikutimiza akidi ya wajumbe, pamoja na kughushi saini ya mjumbe mmoja, ambaye hakuwepo katika kikao hicho.
Baada ya mkanganyiko huo, kesho yake, tarehe 10 Januari mwaka huu, Meya Mwita alienda ofisini kwake kwa ajili ya kuendelea na majukumu yake ya kazi, akisema kwamba bado ni meya halali wa jiji hilo, kwa kuwa mchakato uliotumika kumng’oa haukuwa halali.
Leave a comment