BERNARD Membe, Waziri Mstaafu wa Mambo ya Nje katika serikali ya awamu ya nne, amewekewa ngumu kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Ni kwa kuwa, Chadema kimeweka matumaini yake kwa Tundu Lissu, makamu mwenyekiti wa chama hicho kugomea urais kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Kauli ya kumwekea ‘ngumu’ Membe imetolewa leo tarehe 3 Machi 2020 na Mzee Hashimu Juma, Mwenyekiti wa Baraza la Wazee la chama hicho (BAZECHA).
“Sisi kama wazee tumemridhia na tunampa baraka zetu zote Lissu, kwa hivyo Mheshimiwa Membe tunamtakia kila la kheri na kama atakwenda chama kingine, tutashukuru na tutafurahi kwa sababu kwa vyovyote vile anakwenda kuzigawa kura za CCM.
“Ni kwa sababu, Membe hawezi kuchukua kura hata moja ya Chadema, ataondoka na kundi kubwa la CCM kama Lowasa hivyo atapata kura za chama atachoenda pamoja na za CCM.” amesema Mzee Hashimu.
Hata hivyo, Mzee Hashim amesema, wao hawana uamuzi wa juu wa chama katika kuamua nani atapokewa ama kuteuliwa kugombea urais kupitia chama hicho.
“Sisi ni viongozi wa Baraza la Wazee taifa sio Kamati Kuu, hatuna mamlaka ya kutoa uamuzi wowote lakini kwa mtazamo wetu, sifikiri kama Membe atakuja kwetu.
“Kwasababu, kuna kiongozi wetu maarufu ameshatangaza huko duniani kuwa, kama atapitishwa na Chadema ataipeperusha bendera ya chama chetu kwenye uchaguzi wa urais 2020,” amesema.
Wakati huo huo Mzee Hashimu ameeleza, msimamo wa BAZECHA ni kupigania Tume Huru ya Uchaguzi ili uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2020 uwe wa huru na haki.
Amesema, chama hicho kitafikia mwisho wa uvumilivu tarehe 25 Oktoba kwenye uchaguzi huo kwa kuwa, hawatavumilia kupokwa haki yao.
Leave a comment