TAARIFA za Bernard Membe, aliyekuwa mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, ‘kukimwaga’ chama hicho, zinavuruga wengi. Anaandika Faki Sosi, Dar es Salaam…(endelea).
Tayari mjadala wa taarifa hizo umepamba moto huku chama hicho kijigamba ‘Membe ni mwanachama wetu mtiifu na bado tunaye.’
Akizungumza na MwanahALISI Online kuhusu mjadala unaotikisa kwenye mitandao kwamba, Membe amekipa talaka chama hicho, Ado Shaibu ambaye ni Katibu Mkuu wa chama hicho amesema, ACT-Wazalendo kinapuuza mjadala huo na kwamba hauna afya.
“Taarifa za mitandao tunaziona na ukweli ni kwamba, sisi kama chama tunatambua Membe bado ni mwanachama wa chama chetu,” amesema.
Alipouulizwa kama chama hicho kiliwahi kukutana kujadili chochote kuhusu Memba ama kupokea takwa lolote la mwanachama huyo, amesema hakuna kikao kilichokaliwa.
“Mpaka sasa hakuna kikao chochote kilichojadili chochote kuhusu Membe, na wala hakuna taarifa yoyote kutoka kwa Membe kuja kwenye chama chetu. Mpaka sasa tunapoongea Membe bado ni mshauri wa chama chetu,” amesema Shaibu na kuongeza:
“Sio kila taarifa inayotikisa ama kuibuliwa mitandaoni basi lazima itupeleke resi, chama chetu kina taratibu zake tena zilizo wazi. Nikuhakikishia hakuna mabadiliko yoyote kwa Membe kuwa mwanachama wetu na nafasi yake ya ushauri bado ipo pale pale.”
Membe aliyekuwa mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), alijiunga na ACT – Wazalendo Julai 2020, ambapo aliteuliwa kugombea urais kupitia chama hicho kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020.
Kwenye uchaguzi huo, Membe alishikanafasi ya tatu kwa kupata kura 81,129 sawa na asilimia 0.5, wapili akiwa Tundu Lissu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) aliyepata kura 1,933,271 sawa na asilimia 13 ambapo nafasi ya kwanza alitangazwa Dk. John Magufuli wa CCM aliyepata kura 12,516,256 sawa na asilimia 84.
Wakati kampeni za uchaguzi zikielekea ukingoni, kuliibuka sintofahamu kati ya Membe na viongozi wa chama hicho hasa kutokana na msimamo wa ACT-Wazalendo kumuunga mkono aliyekuwa mgombea urais wa Chadema, Lissu.
Licha ya taarifa za mwenyekiti wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye sasa ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar na Zitto Kabwe, kiongozi wa chama hicho kuwaeleza wanachama wa ACT-Wazalendo kumuunga mkono Lissu, Membe aliendeleza msimamo wa kutaka kuunga mkono na wanachama wa chama hicho.
Hatua hiyo iliibua mvutano kati ya Membe na viongozi wa chama hicho.
Leave a comment