MPAMBANO wa soka wa kufuzu kwa kombe la dunia, kati ya timu ya taifa ya Guinea na Morocco, uliokuwa umepangwa kufanyika jana nchini humo, umeharishwa kufuatia kuibuka machafuko nchini Guinea. Anaripoti Kelvin Mwaipungu… (endelea).
Shirikisho la soka duniani (Fifa), limesema uamuzi huo ulichukuliwa ili kulinda usalama wa wachezaji na maafisa wa mechi.
Timu ya taifa ya Morocco imenaswa nchini humo baada ya mapinduzi hayo na inaripotiwa kungoja kupata idhini ya ubalozi wake kusafiri hadi uwanja wa ndege.
Rais Alpha Condé wa Guinea, ambaye aliingia madarakani mwaka wa 2010 katika uchaguzi wa kwanza ulioshuhudia makabidhiano ya mamlaka ya njia ya amani, alitangazwa mshindi wa kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana, ambao ulidaiwa kugubikwa na udanganyifu.
Licha ya utawala wake kufanikiwa kuboresha hali ya uchumi amelaumiwa kwa kuongoza serikali inayokiuka haki za binadamu na unyanyasaji wa wakosoaji wake.
Mwanasiasa huyo mkongwe kwa sasa, anadaiwa amekamatwa na jeshi linalodai limechukua madaraka ya kuongoza taifa hilo.
Mpaka sasa, hakuna anayefahamu hatima ya rais Condé, kufuatia video ambayo haijathibitishwa kumuonyesha akiwa mikononi mwa wanajeshi, ambao walisema wamefanya mapinduzi.
Hata hivyo, waziri wa ulinzi amenukuliwa akisema, jaribio hilo la kuichukua serikali lilikuwa limeshindwa.
Hii inafuatia saa kadha za makabiliano ya risasi karibu na Ikulu ya rais, katika mji mkuu, Conakry.
Leave a comment