HALIMA Mdee, Mbunge wa Kawe, jijini Dar es Salaam amesema, hakuna wa kumbabaisha kwenye Jimbo la Kawe, kuelekea uchaguzi mkuu wa 2020. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Mdee ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) amesisitiza, mtu wa kumng’oa katika Jimbo la Kawe, hajazaliwa.
Ametoa kauli hiyo leo tarehe 8 Januari 2020, alipoulizwa na MwanaHALISI Online kwamba, inaeleza kuwa na hofu ya kushindwa kwenye jimbo hilo.
Na kwamba, taarifa zinaeleza kuwa hana mpango wa kugombea kwenye jimbo katika uchaguzi mkuu wa 2020, hivyo karata pekee ya kumfanya kuwa mbunge ni kupitia Viti Maalum akiwa Mwenyekiti BAWACHA.
“…mpaka sasa hakuna wa kuniondoa Kawe, hajazaliwa mpaka sasa,” Mdee amesema kwa kifupi akidai, wakati wa kutoa maelezo marefu kuhusu swali hilo, haujafika.
Mdee pia amekitaka Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutorudia iliyofanya kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, kwamba hakitavumilika tena.
“Wasije wakafikiria uhuni wa serikali za mitaa wataufanya kwenye uchaguzi wa madiwani na wabunge. Kwanza huko chini hakukaliki. Wamejipa vyeo kinadharia lakini vitendo Chadema ndio mpango mzima kitaa,” amesema Mdee.
Leave a comment