MBUNGE Viti Maalum asiye na chama bungeni, Halima Mdee, amehoji kinachokwamisha utekelezaji Mpango wa Uboreshwaji Makazi ya Jiji la Dar es Salaam (Dar es Salaam City Master Plan 2016-2036). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, leo Jumanne tarehe 25 Mei 2021, Mdee alihoji lini utekelezwaji mpango huo utaanza, ambao ulipaswa kuanzwa 2012, kisha ukasogezwa mbele hadi 2016.
Mdee amesema mkoa wa Dar es Salaam unakabiliwa na changamoto ya ujenzi holela, na kwamba kama mpango huo ungetekelezwa ipasavyo, ungetatua changamoto hiyo.
“Changamoto ambayo inakumba maeneo menginge ya ujenzi holela, inaikumba Jiji la Dar es Salaam. Tofauti na maeneo mengine, Dar es Salaam tuna City Master Plan ya 2012-2032 ambayo tumeshaipitisha ngazi zote, inasubiri utekelezaji,” amesema Mdee na kuongeza:
“Nataka waziri uniambie, lini Serikali itaanza kutekeleza mkakati huo ili mji wetu upangike vizuri na uondokane na changamoto zote za mji kutokupangwa.”
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula, amesema mpango huo umeshaanza kutekelezwa lakini kasi yake ni ndogo, kutokana na kukwamisha na makazi holela katika mkoa huo.
“Ni kweli Dar es Salaam inayo Master Plan na ilishapitia ngazi zote, lakini changamoto iliyopo ni utekelezaji wake, bado katika halmashauri zinazohusika kufanya kazi kuna changamoto. Sababau utekelelezaji unakwenda awamu kwa awamu, kutegemeana na utaratibu wa mpangilio walioweka,” amesema Mabula.
Mabula amesema “utekelezaji umeanza japokuwa kasi yake ni ndogo, sababu Dar es Salaam imejengeka katika utaratibu ambao sio za kimipango miji katika maeneo mengi. Kwa hiyo lazima twende nao taratibu kulingana na kile ambacho kimepangwa na halmashauri,” amesema Mabula.
Ili kukabiliana na ujenzi holela, Mabula amesema halmashauri za mkoa huo zinaanza kutoa masharti kwa wananchi, wanaokwenda kuomba vibali vya ujenzi, ili wafuate taratibu za mipango miji.
“Lakini kwa sasa utekelezaji wa ujenzi unaoendelea hawaruhusu ujenzi holela, hata katika ujenzi unaoendelea kujengwa nyumba katika maeneo ambayo Master Plan inazungumzia habari ya kwamba kuna maghorofa kadhaa, ukiomba kujenga nyumba ya kawaida unazuiwa,” amesema Mabula.
Leave a comment