MCHUNGAJI wa Kanisa la Evangelist Assemblies of God (EAGT), Nason Manyere, amewashauri Watanzania kujiunga na bima ya afya, ili kuepukana na mzigo wa gharama za matibabu wanapougua. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Mchungaji Manyere ametoa wito huo leo Jumapili, tarehe 20 Juni 2021, akihubiri katika Kanisa la EAGT Uzunguni, jijini Dodoma.
“Nawahamasisha waumini wa kanisa hili pamoja na jamii kwa ujumla, kuhakikisha mnakata bima ya afya kwa mtu mmoja na familia kwa ujumla. Iwapo utakuwa na bima ya afya ni wazi utapata huduma nzuri ya matibabu, pale unapokumbana na matatizo ya kiafya. Bila ya kuwa na mawazo ya kufikiria utapata wapi hela ya matibabu” amesema Mchungaji Manyere.
Mbali na wito huo kwa Wanatanzania, Mchungaji Manyere ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutoa matibabu bora kwa wazee, jambo ambalo lilikuwa changamoto kwa kundi hilo, hasa kwa wasiokuwa na uwezo.
“Tuna kila sababu ya kuwapongeza viongozi wa Serikali, pamoja na Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto, kuhakikikisha wanatoa huduma ya afya kwa wazee, kwa kiwango kinachotakiwa” amesema Mchungaji Manyere.
Wakati huo huo, Mchungaji Manyere amesema, EAGT litaendelea kufanya maombi ya kuliombea Taifa pamoja na viongozi wote waliopo madarakani, ili waendeleze mambo mema ambayo yanaendelea.
“Taifa hili la Tanzania, ni lenye neema na marais waliotangulia wamefanya mambo mazuri, kwa maana yake ni wajibu wetu viongozi wa Mungu na waumini kwa ujumla kumuombea Rais Samia, waziri mkuu, Baraza la Mawaziri, Bunge na mhimili wa Mahakama, ili waendeleze yale mazuri yaliyoachwa na waasisi waliotangulia” amesema Mchungaji Manyere.
Leave a comment