KANISA la Wabaptist Tanzania limewataka viongozi wa serikali pamoja na vyama vya siasa kuhakikisha wanakuwa mabalozi wa kulinda amani ya nchi, anaandika Dany Tibason.
Kauli hiyo limetolewa huku kukiwa na wimbi la kuwapo matukio mbalimbali ya uhalifu yakiwamo ya watu kuvamiwa na kupigwa risasi na ”watu wasiojulikana”
Makamu mwangalizi mkuu wa Kanisa la Wabaptist Tanzania (BCT) Mchungaji, Michael Nhonya, alitoa kauli hiyo wakati alipokuwa akihubiri katika ibada iliyofanyika kanisani hapo eneo la Makole mkoani Dodoma.
Amesema kuwa hali ya wasiwasi inayojitokeza kutokana na vitendo ambavyo vinavyoashiria kupoteza amani ni muhimu vyombo hivyo vikasaidia kudumisha amani ya nchi.
Amesema ili kukabiliana na vitendo hivyo visiendelee kujitokeza kuna haja ya serikali kuingilia kati na kufanya uchunguzi wa kina ili kuwabaini wahalifu hao.
Amesema kuwa kanisa hilo kamwe halitaweza kuvivumilia vitendo hivyo bila kuvikemea.
Ameongeza kuwa bado wanaamini nchi ya Tanzania ni ya amani na utulivu.
“Sisi kama viongozi wa dini tutaendelea kukemea kila mtu bila kujali cheo chake, tutasema na kuelekeza inapobidi kufanya hivyo”, amesema.
Amewataka Watanzania kuwa na subira wakati vyombo vya dola nchini vikiendelea kuchunguza matukio yanayotokea kwa sasa.
Leave a comment