NYOTA wa zamani wa Chipolopolo, Philemon Mulala amefariki dunia baada ya kuumwa na mbwa wake watatu nyumbani kwake Lichtenburg Afrika Kusini. Yameripoti Mashirika ya Habari ya Kimatiafa … (endelea).
Taarifa zinaeleza kuwa Mulala aliumwa na mbwa hao alipotoka nje kuchunguza kwanini walikuwa wanabweka sana baada ya umeme kukatika.
Msemaji wa polisi, Sam Tselanyane, ameiambia BBC kuwa mke wake aliwaambia kwamba alisikia mbwa wakibweka lakini hakujishughulisha na kwenda kuangalia ni nini kilikuwa kibaya kwani mbwa hao mara kwa mara walikuwa wakiwabwekea watembea kwa miguu na magari yaliyokuwa yakipita.
“Baada ya umeme kurudi, aliingia ndani ya nyumba hiyo akimtafuta mumewe lakini hakumpata, baada ya kuendelea na upekuzi, mwanamke huyo alimuona mumewe akiwa amelala nje kwenye bustani. Kisha akatoka nje kupeleleza kulikoni, na akagundua mume wake alikuwa hatikisiki baada ya kuumwa na mbwa wao watatu.”
Mamlaka zimewaondoa mbwa hao wawili ambao ni ‘Cross breed” ya Pitbul na mbwa wa tatu hajulikani asili yake ila anasemekana kuwa mkali.
Mulala alihamia Afrika Kusini kuichezea klabu ya Kaizer Chiefs mwaka wa 1988. Pia alichezea Cape Town Spurs na Lenasia Dynamos.
Shirikisho la soka la Zambia (FAZ)limetoa taarifa ya kuomboleza kifo cha Mulala likisema alikuwa sehemu ya kikosi cha Zambia cha mwaka 1984 kilichoshinda Kombe la East and Central Africa Challenge chini ya ukufunzi wake kanali Brightwell Banda.
Katibu Mkuu wa FAZ Adrian Kashala amesema chama cha soka kimepoteza mchezaji hodari.
Tunabaki na kumbukumbu nzuri ambazo marehemu Philemon alituheshimu nazo uwanjani. Kuna mengi ambayo wachezaji wa leo wanaweza kujifunza kutoka kwa kizazi cha marehemu,” Kashala alisema.
Leave a comment