MBUNGE wa jimbo la Mbozi mkoani Songwe kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Pascal Haonga na wenzake wameshinda kesi iliyokuwa inawakabili katika Mahakama ya Wilaya ya Mbozi, baada ya upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha makosa dhidi ya watuhumiwa. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Haonga na wengine Katibu wake Wilfred Mwalusamba na Mashaka Mwampashi walikuwa wakikabiliwa na makosa ya kuvuruga mkutano wa uchaguzi wa baraza la mji mdogo wa Mlowo kosa la pili na la tatu kuwazuia askari kutekeleza majukumu yao makosa hayo wanadaiwa kuyatenda tarehe 28 Agosti, mwaka huu.
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mfawidhi Nemes Chami alisema katika mashtaka yote matatu yalikuwa yanawakabili, hakuna hata sehemu moja upande wa mashtaka uliothibitisha.
“Hakuna mahali walipoonesha kwamba washtakiwa hawa waliwazuia askari kutekeleza majukumu yao na hakuna mahali walipo thibitisha kwamba washtakiwa walilazimisha kurudi ukumbini baada ya kutolewa nje” Alisema Chami.
Baada ya kusoma hukumu hiyo hakimu huyo alisema kuwa kama kuna upande ambao haujarizika na hukumu hiyo una haki ya kukata rufaa ndani ya muda.