MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM), Christine Mnzava, ameihoji serikali juu ya kutokuwatumia vizuri wanafunzi wanaohitimu shahada ya sayansi ya menejimenti ya uhandisi wa viwanda kwenye uchumi wa viwanda. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea)
Mnzava amehoji hayo leo Jumatano, tarehe 21 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma, akisema wanafunzi wengi waliohitimu katika fani hiyo hawajaajiriwa kuanzia mwaka 2019 hadi 2020.
“Je, ni wanafunzi wangapi waliohitimu katika fani hiyo wameajiriwa Serikalini tangu mwaka 2019 hadi 2020,” amehoji.
Amesema serikali inapaswa kuwatumia vizuri wanafunzi wanaohitimu fani hiyo hususani kuajiliwa kwenye sekta binafsi kwa ajili ya kukuza uchumi wa viwanda.
Akijibu swali hilo, Prof. Kitila Mkumbo, Waziri wa Viwanda na Biashara, amesema, kuanzia mwaka 2017 hadi 2018, wahitimu wa fani hiyo wameajiriwa katika sekta binafsi hususani katika viwanda vya kuzalisha bidhaa.
“Shahada ya sayansi katika menejimenti ya uhandisi wa viwanda yaani (Bachelor of Science in Industrial Engineering Management) ilianzishwa mwaka 2015 katika chuo cha Mzumbe likiwa na lengo kuu moja la kuzalisha wataalamu wa kusimamia shughuli za uzalishaji,” amesema Profesa Kitila.
Leave a comment