MBUNGE wa Viti Maalum, Suzana Mgonukulima (Chadema) amesema anasikitishwa na serikali kutoweza kujibu maswali kwa ufasaha na badala yake wanajibu kisiasa. Anaripoti Dany Tibason … (endelea).
Kauli hiyo aliitoa leo bungeni alipokuwa akiuliza swali la nyongeza kwa kutaka kujua kama serikali ina mpango wa kukwamisha halmashauri ambazo zinaongozwa na upinzani au la kutokana na kutozipatia fedha za maendeleo halmashauri hizo.
Katika swali lake la nyongeza amesema kuwa kwa sasa mapato yanayotokana na makusanyo katika halmashauri yanapekekwa serikali kuu lakini hakuna fedha zinazorudi katika halmashauri kwa ajili ya maendeleo licha ya kuwa halmashauri imekuwa ikiomba fedha kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
Awali katika swali la msingi la mbunge huyo alitaka kujua ni kwanini isitungwe sheria ya kuibana serikali ikiwa haitarejesha fedha za kodi kwenye halmashauri, kwenye miji, Manispaa na Majiji.
“Lengo la Serikali ni kuingiza fedha zote za kodi kwenye mfuko moja kwa moja na baadaye asilimia Fulani ya fedha hizo zirudishwe kwenye halmashauri.
“ Je ni kwanini isitungwe sheria ya kuibana serikali ikiwa haitarejesha fedha za kodi kwenye halmashauri, kwenye miji,Manispaa na Majiji,” alihoji mbunge huyo.
Akijibu swali hilo Naibu Waziri wa Fedha, Dk. Ashantu Kijaji amesema kuwa kwa mujibu wa sheria ya bajeti ya mwaka 2015 kifungu namba 58 usimamizi wa mapato utazingatia misingi mbalimbali.
Aliitaja misingi hiyo kuwa ni mapato yote ya serikali kuingizwa kwenye mfuko mkuu wa serikali, yoyote aliyepewa mamlaka ya kukusanya mapato ya serikali atawajibika ipasavyo katika ukusanyaji wenye ufanisi, utunzaji wa hesabu, utoaji wa taarifa na kuzuia ufujaji wa mapato.
Aina nyingine aliyoitaja Dk. Kijaji ni mapato yote kuingizwa kwenye sheria ya kuithinisha matumizi ya fedha za serikali.
Aidha alisema kuwa kwa mujibu wa kifugungu cha 44 cha sheria ya bajeti, mgawo wa fedha utazingatia bajeti iliyoithinishwa, upatikanaji wa mtiririko wa fedha, utekelezaji mpango wa manunuzi na mpango wa kuajiri.
Leave a comment