MBUNGE wa Mahonda, Unguja, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdullah Mwinyi, ameshauri sheria zinazokandamizi misingi ya demokrasia na utawala bora, zirudishwe bungeni kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho, ili kulinda amani ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Abdullah ametoa ushauri huo leo Ijumaa tarehe 23 Aprili 2021, bungeni, wakati akichangia hotuba ya makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ya mwaka 2021/22.
Akichangia hotuba hiyo, Abdullah amesema: “Ningependa kuzungumzia suala la utawala bora, tumejichagulia sisi kama nchi kuendesha kwa misingi ya demokarsia. Serikali ya watu inayowatumikia wao. Huu ndio mfumo wetu.”
Mbunge huyo ambaye ni mtoto wa aliyekuwa rais wa Jamhuri ya Muungano na Rais wa Zanzibar, Alhaji Ali Hassan Mwinyi amesema, “tuwe tunalinda hii misingi, ili iwalinde watu na mali zao, na misingi hii ilinde utu wao.”
Aliongeza, “kwa mantiki hiyo basi, ningependa kuona sheria ambazo zimetoka nje ya mlolongo huu, nje ya mfumo wa utawala bora ziletwe na tuzirekebishe.”
Abdullah amesema, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alifanikiwa kuwaunganisha wananchi wa pande mbili za Muungano – Tanganyika na Zanzibar, na kuimarisha amani, kwa kuenzi misingi ya utawala bora na kukomesha ubaguzi katika taasisi za umma.

Katika kukazia hoja yake ya ulinzi wa amani, mwanasiasa huyo ametolea mfano kauli ya Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Karagwe, Dk. Benson Bagonza, inayohimiza upatikanaji wa haki kwa ajili ya kuilinda amani.
“Askofu Bagonza anasema, amani ni tunda la haki, na haki hiyo aliitenda Baba wa taifa (Mwalimu Nyerere), kuhakikisha kwamba taasisi zote za Serikali ziko na sura ya kiutaifa, ndiyo zao lake hii amani,” ameeleza Abdullah.
Ameshauri Waziri wa Nchi-Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mohamed Mchengerwa, kuhakikisha anaondoa ubaguzi kwenye taasisi za umma hasa zinazoshughulika na masuala ya Muungano.
“Waziri naomba nikukumbushe hili somo la kihistoria na sina shaka yoyote utalichukulia kwa umakini na katika uboreshaji wenu wa taasisi mtazingatia sura ya kitaifa,” ameeleza na kuhoji, “…na hii ina maana gani?”
Amesema, “Mwalimu Nyerere alichukia ukabila, udini na alihakikisha taasisi za kimuungano zina sura ya kimuungano, hili ni jambo la muhimu ili amani idumu.”
Bunge la Jamhuri linaendelea na mkutano wake wa bajeti mjini Dodoma, ambapo wabunge wanajadili matumizi ya serikali na makadirio na mapato ya matumizi hayo.
Leave a comment