JOSEPH Kasheku (Msukuma), Mbunge wa Geita (CCM), amevutana na serikali kuhusu utaratibu wa Jeshi la Polisi kutumia wanaume kukagua wanawake. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Amelalamika kuwa, jeshi hilo limekuwa likitumia askari wa kiume na utaratibu unaotumika kwenye vituo vingine vya polisi kwenye majimbo mengine.
Akizungumza bungeni jijini Dodoma leo tarehe 24 Juni 2019, Msukuma amepinga majibu ya serikali yaliyokanusha madai hayo, pamoja na sababu za kutopeleka askari wa kike jimboni mwake.
Awali, Mhandisi Hamad Massauni, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi akijibu madai hayo ya Msukuma, amekiri ukosefu wa askari hao, huku akieleza kwamba mazingira magumu na ukosefu wa miundombinu rafiki ya kiutendaji, ni miongoni mwa sababu za serikali kutopeleka askari wa kike kwenye jimbo lake.
Wakati huo huo, Mhandisi Massauni alikanusha madai ya Msukuma kwamba watuhumiwa wa kike hukaguliwa na askari wa kiume, akisema kwamba watuhumiw ahao hukaguliwa na mgambo wa kike au wanawake walioko karibu na vituo vya polisi kwa wakati husika.
Vile vile, Mhandisi Massauni amesema serikali imeshindwa kupeleka askari wa kike katika vituo vya polisi vilivyomo kwenye jimbo la Msukuma, kutokana na jimbo hilo kuwa na mazingira magumu na ukosefu wa miundombinu rafiki ya utendaji kazi kwa askari hao.
Baada ya Mhandisi Massauni kutoa ufafanuzi huo, Msukuma aliibuka na kusema kwamba majibu hayo ni ya uongo hasa sababu za serikali kutopeleka askari wa kike katika vituo vilivyomo jimboni mwake.
Msukuma amesema kuna majimbo yaliyojirani na Geita Mjini ambayo mazingira yake yanafanana, lakini serikali imepeleka askari wa kike.
“Kwanza nisikitike sana kwa majibu yaliyotolewa na naibu waziri hayaendani kabisa na maeneo ya jimbo langu la Geita na kwa bahati nzuri Waziri mhusika Kangi Lugola familia yake wanakaa kwenye jimbo langu na yeye amekaa kwenye jimbo langu anayajua mazingira na majibu yaliyotolewa si sahihi,” amesema Msukuma na kuongeza.
“Mfano ukichukulia kituo cha Nyalugusu, Bwanga na Chato Vijijini, mazingira karibia tunafanana na wana askari wa kike.”
Malalamiko hayo ya Msukuma yalimuibua Lugola, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, na kueleza kwamba ametoa maagizo kwa Jeshi la Polisi mkoani Geita kupeleka askari wa kike katika vituo vya polisi vilivyokosa askari hao.
“Wapo wabunge wnegi wamekuwa wakiomba tuwapelekee askari wa kike, najua askari wa kike wakiwepo katika maeneo mbalimbali ni faraja kwa wananchi kwa sababu huruhusiwa hata kuwapekua watuhumiwa wa kiume, najua Msukuma anatarajia kuona askari wa kike katika maeneo mbalimbali ya vituo vya polisi,” amesema Lugola.
Leave a comment