MBUNGE wa Makete (CCM), Festo Sanga ametaka wawekezaji kwenye mpira wa miguu nchini walindwe na kutoruhusu watu kuwashambulia bila utaratibu wakati michakato yote ya mabadiliko ipo wazi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Sanga ameyasema hayo jana Bungeni wakati akichangia kwenye Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Mbunge huyo ambye alikuwa Mtendaji Mkuu wa klabu ya Singida United, alisema wawekezaji wanapaswa kupewa nafasi ili kufanikisha mambo yao na sio kuwachanganya na mambo madogo madogo yanayoweza kuzungumzika ndani ya timu.
“Wawekezaji walindwe (wanaowekeza Simba na Yanga na klabu nyingine), serikali isiruhusu watu kuwashambulia wawekezaji bila utaratibu, wakati mchakato wote upo wazi na unabaraka zote za Mkutano Mkuu wa Simba na Yanga,” alisema Mbunge huyo na kuongeza.
“Simba ipo vitani ikipambania rekodi ya Africa, lazima tuwape nafasi wafanikishe jambo lao siyo kuwachanganya na mambo madogo madogo ambayo yanazungumzia ndani ya Mikutano halali ya timu.”
Sanga ameyasema hayo kutokana na sintofahamu zinazoendelea hivi karibuni kwa klabu za Simba na Yanga ambazo zinabadilisha mfumo wa uendeshaji wa klabu zao kutoka kwa wanachama hadi kampuni, ili kuruhusu wawekezaji kutoka nje kuja kuwekeza kwa kununua hisa asilimia 49.
Kwa sasa klabu ya Simba ipo hatua ya mwisho ya mchakato huo, huku tayari timu imeshaanza kuonesha mafanikio ndani ya uwanja baada ya Mohammed Dewji ‘MO’ kushinda zabuni kwa kununua hisa asilimia 49 zenye thamani ya bilioni 20.
Kwa upande wa Yanga nao wameshaanza mchakato huo kupitia wafadhili wao kampuni ya GSM na Sanga kusema watu wakiendelea kuwavuruga wawekezaji kama hao mpira wa Tanzania utaendelea kubaki pale pale.
“Hata Yanga ipo kwenye michakato ya uwekezaji, tukiendelea kuruhusu watu wa kuwavuruga wawekezaji kama (GSM) tutabaki palepale tulipodumu kwa miaka 100,” alisema Sanga.
Aidha mbunge huyo alitaka serikali kupunguza kodi kwenye vifaa vya michezo kama nyasi bandia ili wamiliki wa viwanja waweze kufanyia marekebisho viwanja hivyo.
Leave a comment