MBUNGE wa jimbo la Mlimba mkoani Morogoro nchini Tanzania, Godwin Kunambi, ameitaka Serikali kuja na mpango wa kuunganisha umeme bure na kisha kukata gharama hizo kidogo kidogo kwenye bili ya mteja. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Mbunge huyo amesema hilo limekuwa likifanyika katika kuunganisha huduma zingine hivyo linawezekana pia katika sektaya nishati ya umeme.
Kunambi ameyasema hayo leo Alhamisi tarehe 2 Juni, 2022, bungeni jijini Dodoma akichangia hoja hotuba ya bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka 2022/23.
“Kwanini Serikali isije na mpango wa wananchi kuunganishwa bure na kisha kutozwa gharama za kuunganishiwa kwenye bili ya umeme kama ambavyo inafanyika katika huduma zingine?” amehoji Kunambi.
Amesema hatua hiyo itarahisisha zoezi la kuunganishiwa umeme “na wananchi wataona unafuu kwamba anaunganishiwa umeme bila gharama.”
“Kaka yangu (Januari Makamba) najua wewe ni fresh minded na una fikra nzuri nikuombe jambo hili ukilifanya utapata credit na serikali itaongeza mapato.”
Katika hatua nyingine Kunambi ameshauri ununuzi wa LUKU uwe wa moja kwa moja kama ilivyo katika ununuzi wa vifurushi vya ving’amuzi.
Amesema hiyo itasaidia mtu kuingiza umeme katika mita kupitia simu yake akiwa sehemu yeyote nchini bila kulazimika kwenda kuingiza namba za tokeni kwenye mita.
Akizungumzia mradi wa REA amesema jimboni kwake unatekelezwa kwenye vijiji 11 lakini kuna changamoto wa mkandarasi kutoanza kazi mapema.
“Hata mashimo hajachimba na hata nguzo hajaleta wasiwasi wangu mmesema mradi utakamilika Desemba lakini mkandarasi anaweza kuja kuomba extension ya muda,” amesema Kunambi.
Kuhusu utafiti wa mafuta na gesi Kunambi amesema Tanzania ina uwezo wa kuwekeza na kwamba changamoto sio fedha bali ni uzalendo, mtazamo na uwajibikaji.
“Jambo hili linawezekana nchi yetu ni Tajiri hatuna changamoto ya fedha changamoto kubwa ni uzalendo na mindset na uwajibikaji,”
“Uwezo wako naujua na naibu wako na naamini mna katika hili mna nafasi badoo kwa kutumia mambo haya matatu tunaamini mtakwenda kufanya mambo makubwa sana,” amesema Kunambi.
Leave a comment